Sunday, July 24, 2011

Nishati wafanya ufisadi kwa miaka minne

YABAINIKA JAIRO ALIHUSIKA MIAKA MIWILI, KAFULILA AWASHTAKI KWA JK
Neville Meena, Dodoma
IMEBAINIKA uchotaji wa mamilioni ya fedha katika Idara na taasisi za umma zilizoko chini ya Wizara ya Nishati na Madini kugharamia shughuli zinazohusiana na gharama za bajeti ya wizara hiyo, ulianza mwaka 2004.

Kuanzia Julai 2008, kila mwaka Ofisi ya Katibu Mkuu katika wizara hiyo imekuwa ikiandika barua kwa wakuu wa taasisi hizo kutaka fedha ambazo kwa namna moja au nyingine zinahusishwa na shughuli za bajeti ya wizara kusomwa bungeni au kughramia sherehe ambazo hufanyika baada ya kupitishwa kwa bajeti husika.

Fedha hizo kwa mujibu wa nyaraka husika, zimekuwa zikitumika kugharamia tafrija mara baada ya bajeti kupitishwa na bunge, posho za vikao, posho za kujikimu, vyakula, vinywaji na mafuta ya magari.

Hata hivyo mmoja wa watumishi wa idara ambazo zimekuwa vinara wa kudaiwa fedha wakati wa bajeti alilithibitishia Mwananchi Jumalipi kwamba, wakati wa vikao vyote vya Bunge kila taasisi huwagharamia watumishi wake wanaokwenda Dodoma.

"Mara nyingi wakati wa vikao vya bajeti huwa nakuja hapa Dodoma, lakini utaratibu wa kukaa hapa lazima nijaze fomu ofisini na ipitishwe kwa mabosi wangu ndipo napewa fedha za kuishi, wizara hawawezi kukupa hela," alisema mtumishi huyo na kuongeza:

"Sana sana hapa tukiwa na kazi huwa tunakunywa chai na luch (chakula cha mchana) na hii siyo kila siku, ni kama tuna kazi zinazotuunganisha na wenzetu kutoka ofisi nyingine na maofisa wa wizara."

Matumizi mabaya ya fedha hizo za umma yamebainika kipindi ambacho Katibu Mkuu wa sasa wa Wizara hiyo, David Jairo, amesimamishwa na Ikulu kwa kupewa likizo ya malipo, ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizotolewa bungeni dhidi yake.

Jairo anakabiliwa na tuhuma za kuwaandikia barua wakuu wa idara zote zilizoko chini ya wizara yake, ili watoe fedha kwa ajili ya kusaidia kupitishwa kwa bajeti ya wizara hiyo, fedha ambazo zinatafsiriwa kwamba zilikuwa ni kwa lengo la kutoa rushwa kwa wabunge.

Kafulila ashtaki kwa JK
Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila(NCCR - Mageuzi), jana aliliambia Mwananchi Jumapili kuwa amemwandikia barua Rais Jakaya Kikwete akitaka uchunguzi utakaofanywa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali katika Wizara ya Nishati na Madini uanzie miaka ya mitano iliyopita.

"Nimemwandikia barua Rais Kikwete, maana inaonekana kuwa huu mchezo wa kuchota fedha za Umma katika wizara hii umeanza tangu 2008," alisema Kafulila ambaye pia aliwahi kuwalipua baadhi ya wabunge wenzake, akiwatuhumu kwamba waliomba rushwa katika
Halmashauri ya Handeni, mkoani Tanga.

Kafulila katika barua yake ambayo pia Mwananchi limeiona, alisema anakubaliana na hatua za awali za kumchunguza Jairo, lakini anapendekeza ufanyike uchunguzi mpana kwani mtindo si kwa mwaka huu pekee bali hata miaka iliyopita katika wizara hiyo na nyingine nchini.

"Napenda kupendekeza kwako kuwa suala hili lifanyiwe uchunguzi mpana kwa kuwa upana wa kashfa hii ni zaidi ya mwaka mmoja wa fedha 2011/2012, ni zaidi ya Katibu Mkuu mmoja, David Jairo na pengine ni zaidi ya wizara moja ya Nishati na Madini, katika hicho kinachoelezwa kuwa ni kusaidia uwasilishaji wa bajeti," inaeleza sehemu ya barua hiyo.

Katika barua yake kwa Rais na kutoa nakala kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Spika wa Bunge, Anne Makinda, Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Uttoh na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru), Kafulila anasema ana ushahidi unaothibitisha baadhi ya tuhuma hizo.

Uzoefu wa Jairo
Kwa mujibu wa nyaraka ambazo Mwananchi limeziona, hii ni mara ya pili kwa Jairo akiwa Katibu Mkuu katika wizara hiyo kuandika waraka wa kuomba fedha kutoka kwenye idara husika kwa ajili ya kusaidia mchakato wa maandalizi na uwasilishaji wa bajeti bungeni.

Kwa mujibu wa nyaraka hizo, Mei 12, mwaka jana Jairo akiwa Katibu Mkuu, aliandika waraka kwenda kwa aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Stephen Mabada akitaka lichangie Sh20 milioni ili kusaidia kile alichokiita, ‘Gharama za kukamilisha mpango na bajeti ya wizara 2010/2011 na uwasilishaji wake bungeni."

Barua kama hiyo pia iliandikwa kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Maji na Nishati (Ewura), Haruna Masebu, ambaye taasisi yake iliombwa kuchangia Sh25 milioni, wakati Yona Killagane ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC), taasisi yake ilitakiwa kuchangia Sh20 milioni.

Kwa mujibu wa barua hizo, gharama husika kwa ajili ya kazi hiyo ya kibajeti ilikuwa ni Sh186.6 milioni hivyo kuzitaka idara zote kwa pamoja kuchangia kiasi cha Sh90 milioni, wakati wizara ilibaki na jukumu la kuchangia kiasi cha Sh96.6 milioni.

Hata hivyo jumla ya fedha zilizoombwa kutoka Ewura, Tanesco na TPDC ni Sh65 milioni, ikimaanisha kuwa ipo idara au taasisi nyingine ambayo pia iliombwa kuchangia kiasi kilichobaki cha Sh25 milioni.

"Gharama hizi kubwa zimesababishwa na kupanda kwa gharama za posho kutoka Sh60,000 mpaka Sh200,000, Sh50,000 hadi Sh150,000 na Sh30,000 hadi Sh100,000 kwa wenyeviti na makatibu, wajumbe na sekretarieti sawia," inaeleza sehemu ya waraka huo uliondikwa na Jairo na kuongeza:

"Kwa kuwa bajeti ya wizara ya 2009/2010 ilikadiriwa kwa viwango vya zamani, ni dhahiri wizara haiwezi kubeba gharama hizi peke yake. Hivyo inashauriwa Wizara igharamie 96,626,000 na wadau muhimu wa wizara wagharamie 90,000,000".

Barua hiyo haifafanui kuhusu wenyeviti, makatibu, wajumbe na sekretarieti ambao wanapaswa kulipwa posho hizo.

Miaka iliyopita
Mwananchi limethibtisha kuwa "utaratibu" huo wa kuchota fedha umekuwepo kwa muda mrefu, kwani mwaka 2008 na 2009 Wizara hiyo iliandika barua kwa ajilia kutaka "ichangiwe" ili kughramia shughuli za kibajeti.

Julai 5, 2008 aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Arthur Mwakapugi, aliandika wakara kwa Dk Idris Rashid, aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Lutengano Mwakahesya na Killagane wa TPDC akitaka mchango wa kile alichoeleza kuwa ni
"Kuchangia gharama za hafla fupi baada ya mawasilisho ya bajeti ya wizara bungeni Dodoma".

Katika waraka wake huo, Mwakapugi alitaka kila taasisi kuchangia kiasi cha Sh5 milioni, hivyo kufanya jumla yake kuwa Sh15 milioni kwa lengo la kugharamia tafrija husika.

Juni 19, 2009 Mwakapugi aliandika waraka mwingine kwenda Tanesco, REA na TPDC akitaka michango kwa ajili ya kile alichokieleza katika barua yake kuwa ni "Fedha kwa ajili ya kuwezesha uwasilishaji wa hotuba ya bajeti ya 2009/2010 bungeni Dodoma, kazi ambayo anasema katika barua hizo kwamba, gharama zake ni Sh170,461,500.

"Kama ilivyo desturi, maofisa, taasisi na mashirika yaliyo chini ya wizara hujumuika katika kutoa michango yao hasa katika hoja zote zinazojitokeza katika maeneo husika. Ili kufanikisha zoezi hilo, gharama mbalimbali huhitajika zikijumuisha, posho za vikao, uchapishaji wa vitabu, uchapishaji kwenye magazeti, vyakula na vinywaji posho za safari na mafuta kwa washiriki," inaeleza sehemu ya barua.

Barua hiyo inabainisha kuwa msingi wa kutaka kuchangiwa ni kutokana na hali mbaya kifedha katika wizara hivyo na kuwataka Tanesco kuchangi Sh40 milioni, REA Sh30 milioni na TPDC Sh40 milioni.

Likizo ya Jairo
Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo ambaye ni Mkuu wa Utumishi wa Umma aliwaambia waandishi wa habari mjini Dodoma Alhamisi wiki hii kuwa Jairo ambaye yuko chini yake, analazimika kwenda likizo kuanzia juzi ili kupisha uchunguzi wa awali ambao unalenga kubaini iwapo ametenda kosa la kinidhamu kwa mujibu wa sheria zinazoongoza Utumishi wa Mmma.

Mbunge wa Kilindi (CCM), Beatrice Shellukindo ndiye aliyemlipua Jairo Bungeni Julai 18, 2011 wakati akichangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini akisema amekusanya fedha kiasi cha Sh1 bilioni kutoka idara 21 zilizopo chini ya Wizara yake, fedha zisizo na maelezo.

"Nimeanzisha uchunguzi wa awali kwa lengo la kupata ukweli kuhusu tuhuma hizo. Wakati uchunguzi huo ukiendelea, Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini amepewa likizo ya malipo kupisha uchunguzi wa awali," alisema Luhanjo na kuongeza:

"Hatua zitakazochukuliwa hapo baadaye zitategemea matokeo ya uchunguzi wa awali".

Licha ya mchakato wa hatua dhidi ya mtumishi huyo wa umma ambaye ni mteule wa Rais kupitia katika mchakato mrefu, mwishoni mwa mchakato huo anaweza kushushwa cheo, kupunguzwa mshahara, kufukuzwa kazi, kuachishwa kazi au kurejeshwa kazini kwa kutegemea matokeo ya taratibu zitakazofuatwa.

Luhanjo alisema Jairo analazimika kwenda likizo kwa kuwa tuhuma dhidi yake ni nzito. "Zingekuwa tuhuma nyepesi ningeruhusu aendelee na kazi wakati uchunguzi huo wa awali ukifanyika, lakini tuhuma hizi ni nzito mno. Hivyo lazima aende likizo ili kupisha uchunguzi huo," alisema Luhanjo.

Alisema uchunguzi dhidi ya Jairo kwa kuwa unahusu masuala ya fedha, utafanywa na Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ambayo inatakiwa kikamilisha kazi yake katika muda wa siku kumi kisha kuiwasilisha kwake kwa hatua zaidi.

Taarifa ya Luhanjo ambayo ni taarifa rasmi ya Serikali inatofautina na kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwamba suala la kuchukua kwa hatua dhidi ya Jairo linamsubiri Rais Kikwete ambaye alikuwa katika ziara ya kikazi nchini Afrika ya Kusini.

Seneta wa Marekani aahidi kusaidia wafugaji


Joseph Lyimo,Simanjiro
SENETA wa Jimbo la Oregon, nchini Marekani, Jacks Winter, ameahidi kuboresha miundombinu katika Kijiji cha Lengasti, wilayani Simanjiro,ili kuziwezesha jamii za wafugaji kuondokana na matatizo yanayowakabili.

Seneta Winter alitoa ahadi hiyo juzi alipokuwa akizungumza na wakazi wa kijiji hicho, kilichoko katika Kata ya Naisinyai.

Alisema kwa kushirikiana na watu wa jimbo lake, atahakikisha kuwa wananchi wa Lengasti wengi wao wakiwa ni jamii ya wafugaji, wanapiga hatua za kimaendeleo.

Winter alisema lengo la ziara yake katika Wilaya ya Simanjiro, lilikuwa ni kujifunza mambo mbalimbali ya jamii na kutambua matatizo yanayowakabili wananchi wake.

Alisema tayari ameshajifunza mambo mengi ikiwa ni pamoja na namna ya kuwasaidia wananchi wa eneo hilo, kuondokana na matatizo.Seneta Winter alisema kwa kushirikiana na watu wa Jimbo la Oregon, atahakikisha wananchi wa Lengasti wanatengenezewa miundombinu bora.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Naisinyai, Kilempu Ole Kinoka, alimshukuru seneta huyo kwa kuwachimbia wananchi mabwawa mawili yanayoyatumiwa kwa shughuli za jamii na mifugo.

Alisema kwa sasa wakazi wa kijiji hicho, wanakabiliwa na tatizola ukosefu wa nishati ya umeme kwa ajili ya kuendeshea mtambo wa kuvutia maji ya kunywa na matumizi mengine.

"Huko nyuma wanawake katika kijiji hiki walikuwa wanasafiri kwa umbali wa kilometa 15 wakitafuta maji, lakini sasa maji tatizo hio limepungua hasa baada ya kuchimbiwa mabwawa mawili,"aisema.

Kenya yaomba Tz iruhusu usafirishaji wa mahindi

Rehema Matowo, Moshi
WAKUU wa Wilaya za Taveta na Lotokitok, nchini Kenya, wameiomba Serikali ya Tanzania kuruhusu wafanyabiashara wa mazao ya chakula wa nchi hiyo jirani, kuingia nchini kwa lengo la kununua chakula ili kukabiliana na upungufu mkubwa chakula unaoikumba Kenya kwa sasa.

Rai hiyo ilitolewa juzi na Mkuu wa Wilaya ya Taveta, Nkaduda Hiribae, alipokuwa akizungumza katika kikao cha ujirani mwema, kilichofanyika mjini Moshi.

Kikao hicho kiliwahusha wakuu wa wilaya hizo za Kenya na wakuu wa wilaya za Mkoa wa Kilimanjaro, ambao kwa pamoja, walisaini maazimio yanayotokana na kikao cha kudhibiti uhalifu mipakani, kilichofanyika Julai 13 mwaka huu, katika eneo la Holili, wilayani Rombo.

Hiribae alisema Serikali ya Kenya inaunga mkono agizo la Serikali ya Tanzania kuhusu kudhibiti usafirishaji wa chakula kwenda nje ya nchi, lakini ni vyema serikali hiyo ikaona umuhimu wa kusaidia majirani pale wanapokabiliwa na baa la njaa.

Alisema kwa sasa Kenya inakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula uliofikia kiwango cha asilimia 70, hali ambayo ni tishio kwa usalama wa maisha ya wananchi.

Aliiomba Serikali ya Tanzania, kufungua milango kwa wafanyabiashara wa Kenya, kuingia nchini na kununua chakula kwa njia halali, jambo ambalo pia litaipatia mapato serikali.

Akizungumzia ombi lililotolewa na Hiribae ,Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Alhaji Musa Samizi, alisema wao kama wakuu wa wilaya, hawana mamlaka ya kutoa vibali vya kuruhusu wafanyabiashara wa Kenya na Tanzania kununua chakula na kukiuza Kenya.

Alisema wanachoweza kukifanya ni kuwasiliana na ofisi ya Waziri Mkuu na kufikisha ombi hilo kwa utekelezaji.

Kuhusu maazimio waliyoyaazimia mwenyekiti wa kikao hicho, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Rombo, Peter Toima, alisema ni pamoja na pande zote mbili kushirikiana katika kutoa taarifa zitakazosaidia kuzuia uvushaji haramu wa chakula na uhalifu mwingine.

Alisema azimio lingine ni kuangalia namna wakuu wa wilaya hizo watakavyowasiliana na wizara za Chakula katika pande zote mbili, ili kuona ni jinsi Serikali ya Tanzania inavyowaruhusu Wakenya kununua chakula kutika nchini hata kwa muda mfupi ili kutatua tatizo la njaa linalokabili Kenya.

Mwenyekiti huyo alisema maazimio mengine ni kuanzishwa kwa soko la mazao katika maeneo ya karibu na mpaka wa Holili na Himo ili kuwezesha wafanyabiashara kutoka Kenya, kuja kununua mazao kwa kupitia njia halali na kulipa kodi.

Alisema pamoja na kuazimia kuanzishwa kwa soko la mazao pia wameazimia kufuatilia kwa pamoja maghala yote yaliyoko katika maeneo ya mipakani na kuyachunguza kwani mengi yamekuwa yakitumika kuhifadhia magendo na hata wahalifu.

Warioba asema Bunge limekosa nidhamu

Mwandishi wetu

WAZIRI Mkuu Mstaafu, Joseph Warioba, amesema Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limekosa nidhamu na kwamba, linahitaji kuchukua uamuzi mgumu kurejesha hadhi yake.
Warioba alisema hivi sasa chombo hicho cha kutunga sheria kimegeuka kuwa sehemu vichekesho badala ya kujadili masuala muhimu ya kitaifa.
“Bunge limegeuka kuwa sehemu ya vichekesho, limekosa nidhamu linahitaji kuchukua uamuzi mgumu,” alisema Warioba.
Warioba ambaye alikuwa akizungumza na Televisheni ya Taifa (TBC1) jana asubuhi hakueleza kwa undani ukosefu wa nidhamu wa Bunge hilo.
Hata hivyo, matukio ya kila mara yanayoendelea kutokea bungeni ikiwamo kuzomeana, kuzungumza ovyo bila mpango na kuwapo kwa madai ya rushwa ni moja ya mambo yalimfanya atoe kauli hiyo.
Vurugu zinazotokea bungeni mara kadhaa zimekuwa zikimfanya Spika na wenyeviti wa vikao vya Bunge kuwa katika wakati mgumu kusimamia mijadala.
Mara kadhaa Spika amekuwa akisikika akikemea tabia hiyo hadi wakati fulani alifikia kuwalingananisha na watu wa sokoni Kariakoo.
Hata hivyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alisema wabunge kusingana bungeni si jambo la jabu sana na kwamba ni dalili ya kuelekea kwenye demokrasia kamili bungeni.
Warioba ni Waziri Mkuu Mstaafu wa kwanza kulinyoshea kidole moja kwa moja Bunge katika siku za hivi karibuni.
Moja ya kashfa ambazo hivi karibuni zimelighubika Bunge ni pamoja na baadhi ya wabunge kutuhumiwa kuchukua rushwa ili waweze kupitisha bajeti na miongoni mwa zilizotajwa ni ya Wizara ya Nishati na Madini.
Kashfa hiyo ndiyo iliyosababisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, David Jairo, kuingia katika kitanzi cha kuhusishwa kwake na kuandika barua kwenye taasisi zilizo chini ya wizara yake kuomba fedha za kupitisha bajeti hiyo.
Kashfa nyingine ya Bunge ni lile tukio la wabunge kuzomeana na kumfanya kila mbunge kuwasha kipaza sauti kuongea bila ya kufuata taratibu.
Lawama nyingine dhidi ya Bunge ni ile iliyoibuliwa na Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje ya kutuhumu Kamati ya Bunge kuwa ilifanya mambo kinyume cha taratibu.
Zipo hoja nyingine ambazo ziliibuliwa na kusemwa bungeni zikionya kuwa, Bunge limekuwa likitumika kama ‘rubber Stump’ (mhuri) ya kupitisha mambo mbalimbali bila kuyafanyia uchunguzi wa kina na kujiridhisha.
Warioba akizungumzia Katiba Mpya alisema muswada uliopo katika mchakato umesahau mambo muhimu, kama vile ya uchumi na maendeleo ya jamii badala yake una mambo mengi ya kisiasa.
Alisema masuala mengi yaliyomo ndani ya muswada huo yanalenga kulinda maslahi ya wanasiasa na kuacha kuzungumzia masuala muhimu kwa maendeleo ya wananchi.
Warioba ambaye pia ni Jaji Mstaafu, mara kwa mara amekuwa akitoa kauli nzito za kuishauri Serikali katika masuala ya rushwa na utawala bora.
Mwaka jana, Jaji Warioba alionya dhidi ya mwelekeo wa uongozi nchini kununuliwa kama bidhaa kutokana na vitendo vya rushwa vilivyokuwa vikifanyika karibu na Uchaguzi Mkuu.
Alisema: “Kwa jumla sasa uongozi wa nchi unaanza kubinafsishwa kama biashara ambayo wenye fedha ndiyo watafaulu. Kwa kifupi fedha
SOURCE:Mwananchi

IGP Mwema apangua makamanda

Na Daniel Mjema

INSPEKTA Jenerali wa Polisi (IGP), Said Mwema, amefanya mabadiliko ya safu ya uongozi wa makamanda wa polisi kwa baadhi ya mikoa ya Tanzania bara.

Katika mabadiliko hayo, baadhi ya makamanda wa mikoa wamehamishwa huku maofia 122 wakipandishwa vyeo.

Mabadiliko hayo yameambatana na uteuzi wa vyeo vya juu ambapo Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Tanzania, Rais Jakaya Kikwete, amewapandisha vyeo maofisa watano na kuwa Manaibu Kamishina.

Miongoni mwa waliopandishwa vyeo kutoka kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi(SACP) kuwa Manaibu Kamishina ni pamoja na Kamanda Simon Sirro.

Habari za uhakika ambazo Mwananchi Jumapili inazo zimesema katika mabadiliko hayo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Sirro amehamishiwa makao makuu ya Polisi Jijini Dar kuwa mkuu wa operesheni maalumu za Jeshi hilo.

Nafasi ya Kamanda Sirro imechukuliwa na aliyekuwa kamanda wa Polisi mkoa Tabora, Leberatus Lyimo, huku Ofisa Mnadhimu wa Polisi namba moja wa mkoa huo, Anthony Rutashugurugukwa, akiteuliwa kuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo.

Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Tabora(OCD), Yusuph Mruma, ameteuliwa kuwa Ofisa Mnadhimu namba moja wa Mkoa wa Tabora kuchukua nafasi ya Rutashugurugukwa.

Taarifakuhusu mabadiliko hayo iliyotolewa na IGP Mwema Julai 22 mwaka huu ambayo Mwananchi Jumapili imefanikiwa kuiona, inaeleza pia kuwa tume ya utumishi wa polisi na Magereza imewapandisha vyeo maofisa 117.

Kulingana na taarifa hiyo, maofisa 21 waliokuwa na vyeo vya warakibu wasaidizi waandamizi wa jeshi hilo (SSP), wamepandishwa vyeo na kuwa makamishina wasaidizi wa polisi(ACP) na kuwahamisha vituo vyao vya kazi.

Halikadhalika maofisa 96 waliokuwa na vyeo vya Mrakibu wa Polisi (SP) wamepandishwa vyeo na kuwa warakibu waandamizi wa polisi (SSP).

Baadhi ya waliohamishwa ni OCD Monduli, Contantine Maganga na Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Moshi, Zakaria Benard, wanaohamishiwa ofisi ya Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro ambapo watapangiwa majukumu mapya.

Wengine ni Kihenya Kihenya, ambaye ni OCD Kasulu aliyehamishiwa Mkoa wa Kigoma kuwa Ofisa Mnadhimu namba moja na Alicheus Mtalemwa, ambaye ni Ofisa Mnadhimu namba moja wa Kigoma anakuwa Ofisa Polisi Jamii mkoa Rukwa.

Katika taarifa hiyo ya kipolisi, IGP Mwema amewapongeza maofisa wote waliopandishwa vyeo na Tume ya polisi na Magereza na kwamba upandishwaji huo wa vyeo ulianza rasmi Juni 30 mwaka huu.

Msemaji wa jsehi hilo, Advera Sinso alithibitisha taarifa hizo, lakiniakasema: "Mi mabadiliko ya kawaida tu ya ndani."

Hakuweza kuweka wazi juu ya mabadiliko hayo kwa kile alichodai yuko Dodoma, nje ya makao makuu ya polisi ambayo yapo Dar es Salaa, hivyo akashauri afuatwe kesho.

Mandojo na Domokaya Baada ya kimya kingi, waibukia Fiesta 2011


Herieth Makwetta,
WASANII wakongwe wa muziki wa kizazi kipya, Joseph Francis Michael 'Mandojo' na Precioust Juma 'Domokaya', walikuwa kivutio kikubwa kwa mashabiki wa burudani ya muziki mjini Moshi na Arusha kwenye tamasha la Serengeti Fiesta wiki iliyopita.

Pamoja na kuwepo kwa idadi kubwa ya wasanii waliopanda jukwaani kwenye tamasha hilo, Wawili hao ambao waliwahi kutamba na kibao cha Wanokonoko mwanzoni mwa miaka ya 2000 walichomshirikisha Lady Jay Dee, walitumbuiza jukwaani kwa muda wa dakika 45 pasipo kuwachosha mashabiki.

Hii ni nadra sana hasa kwa wasanii wetu wa hapa nchini kwani wengi wao wamekuwa ni wavivu pindi wawapo jukwaani na wengine wamediriki kuimba bila hisia wala hamasa kwa mashabiki wanaowapenda.

Inaweza ikawa ni dalili kwamba muziki wa kizazi kipya unapoteza mwelekeo, kwani umahiri wa wasanii wakongwe unajionyesha hadharani na kupendwa zaidi na mashabiki ukitofautisha na ule wa chipukizi.

Katika mahojiano na wasanii hawa waliweza kunieleza mawili matatu ambayo huenda ni maswali ambayo msomaji ulikuwa ukijiuliza kwa muda mrefu.

Mwandishi: Imekuwa ni kama 'suprise' kuwaona hapa jukwaani ilikuwaje mbona ni kama mlipotea kwenye fani?

Domokaya: Ni muda mrefu sasa hatujawa kwenye fani, lakini si kwamba tumeacha muziki, bado tunafanya vema. Imekuwa kama kuwashtua mashabiki lakini si kwamba hatuwezi tena muziki ni wazi tumefanya vizuri na nadhani wengi wameona nini tumefanya.

Mwandishi: Lakini ni kweli kwamba bado mna nguvu za kupambana na wasanii chipukizi?

Mandojo: Ng'ombe hazeeki maini. Bado tuna nguvu na kuhitajika na mashabiki. Chipukizi wana nafasi yao lakini hata sisi pia tuna nafasi zetu. Inapopatikana nafasi kama hii lazima tuhakikishe tunafanya kile ambacho tumekubaliana kimkataba na si lelemama.

Domokaya: Unajua linapofikia suala kama hili, bila shaka hatuachi nafasi kubwa kati yetu na promota ambaye ametupa kazi. Hili ni tatizo ambalo wasanii wengi chipukizi wanalo, hawathamini ile nafasi wanayopewa na mapromota hawa wanaoandaa matamasha likiwemo hili la Fiesta, ni heshima kubwa. Hivyo lazima uhakikishe unawafanya mashabiki wako wakuone unafaa na kukonya nyoyo zao.

Mwandishi: Mnadhani muziki wa bongofleva kwa sasa umepoteza mwelekeo?

Domokaya: nadhani ni wakati mzuri kwa wapembuzi wa masuala ya burudani ya muziki kutambua kwamba wakongwe wana nafasi kubwa sana kuliko chipukizi kwa sasa, kwani bongo fleva ya zamani zi ile ya sasa kwani inadumu na haipotezi ladha.

Mandojo: Kwa upande wangu naona umepoteza mwelekeo, kwani sisi tuliimba mapenzi lakini yenye kufundisha na hata nyimbo zingine hazikuwa mapenzi lakini zilielimisha na kufundisha lakini kwa sasa mtu akiimba wimbo mapenzi yanazidi sana, licha ya hivyo bado hazikai zinachuja mapema.

Mwandishi: Mmesema kuwa mmerudi tena kwenye fani mmejipanga vipi.

Mandojo: Tuliwahi kuimba na Lady Jay Dee mwanzoni mwa miaka ya 2000 wimbo wa wanoknok, lakini hivi sasa tutarudi tena tukiwa na Jide na tunategemea kutoa kazi ambayo itakonga nyoyo za mashabiki.

Mwandishi: Bado mnaimba kwa vinanda kama zamani au?

Domokaya:Hapana kwa sasa tunafanya 'live band', kila siku ya Alhamisi tupo pale Nyumbani Loung kwa Jay Dee. Muda mwingi tumekuwa tukiandaa kazi zetu ambazo tunatarajia kuziachia mapema mwaka huu, kwa hiyo mashabiki wakae mkao wa kula.

Mandojo: Tumeandaa nyimbo kama 'Baba Kidawa' ambao tumetengeneza katika studio ya 'Marko Chali' tukiwa katika kundi la Wamandavaku ambalo tumewaingiza vijana wawili.

Mwandishi: Hii inamaanisha kwamba kwa sasa kundi la Mandojo na Domokaya halipo na badala yake kuna Wamandavaku?

Mandojo: Hapana, sisi tutabaki kuwa kama sisi na kundi ni baadaye.
Mwandishi: Je mna lolote la nyongeza?.
Man na Domo: Zaidi ni kuwajulisha washabiki wetu kuwa tumerudi upya waje washuhudie mambo yetu.
Mwandishi: Kazi njema
Man na Domo: Pamoja

Ripoti Maalumu:Tuhuma za rushwa zaivuruga Kamati ya Mrema

Neville Meena, Dodoma
RUSHWA inayodaiwa kupenyezwa kwa baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), imeathiri uamuzi wa baadhi ya hatua ambazo kamati hiyo inapaswa kuchukua dhidi ya udhaifu uliobainika katika hesabu za fedha na miradi inayotekelezwa na halmashauri ambazo tayari zimefanyiwa ukaguzi.

Kwa kawaida kamati hiyo inapofanya ziara katika halmashauri kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake, hubainisha udhaifu katika maeneo husika na kutoa mapendekezo au hatua zinazopaswa kuchukuliwa dhidi ya udhaifu husika na wakati mwingine hutoa au kupendekeza adhabu wanazopaswa kupewa wahusika.

Sehemu ya tatu ya nyongeza ya nane ya Kanuni za Bunge, toleo la mwaka 2007 inabainisha kuwa LAAC ina wajibu wa kushughulikia maeneo yenye matatizo sugu ya matumizi mabaya ya fedha za Serikali za Mitaa yaliyoainishwa katika taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

"Kushughulikia maeneo yenye matatizo sugu ya matumizi mabaya ya fedha za Serikali za Mitaa yaliyoainishwa katika Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali," kinaeleza kipengele cha 12(a) cha sehemu hiyo.

Hata hivyo, uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa taarifa ya Kamati ndogo ya LAAC, iliyokuwa mkoani Tanga kwa ajili ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo, Mei 22- 28, 2011 inatia shaka kutokana na tofauti kubwa ya mapendekezo yaliyotolewa dhidi ya udhaifu uliobainishwa katika muhtasari wa kumbukumbu za kamati hiyo.

Kutokana na udhaifu wa taarifa hiyo, baadhi ya wajumbe ambao walikuwa katika msafara huo wa Tanga wameikana wakidai kwamba wajumbe waliopewa kazi ya kuiandika, 'waliichakachua'.

"Hii ripoti iliandikwa na (anawataja wabunge wawili), nasikia hata Mwenyekiti (Augustino Mrema) hakuwapo kutokana na dharura lakini tuliwaamini, ila walichoandika wanakijua wenyewe," alilalamika mmoja wa wajumbe wa kamati.

Kwa mujibu wa muhtasari huo, kamati hiyo ndogo iliyoongozwa na Mrema kwenda Tanga ilibainisha udhaifu katika vipengele kumi na moja kwenye miradi ya Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto na kutoa mapendekezo 10 ya namna ya kuchukua hatua.

Kadhalika, kamati hiyo inatoa maelekezo kwa lugha kali na kupendekeza hatua za kinidhamu kwa baadhi ya watendaji wa halmashauri za wilaya Muheza na Jiji la Tanga kutokana na kubaini uzembe katika usimamizi wa baadhi ya miradi ya maendeleo inayosimamiwa na mamlaka hizo. Lakini, jambo linalotia shaka ni jinsi kamati hiyohiyo ilivyoshughulikia matatizo yaliyojitokeza katika Halmashauri ya Wilaya ya Handeni kwani ilibainisha upungufu uliowekwa katika vipengele 12, lakini ikatoa mapendekezo matatu tu ya jumla ya jinsi ya kukabiliana na kasoro hizo.

Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo alisema "udhaifu" unaobainika katika uandishi wa hatua za kuchukua dhidi ya watendaji wa Handeni, unaweza kuwa uthibitisho wa tuhuma zilizotolewa dhidi ya baadhi ya wajumbe wa LAAC kwamba waliomba rushwa kwa uongozi wa halmashauri hiyo.

Tuhuma hizo ni zile zilizotolewa Juni 13, mwaka huu na Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila ambaye pia ni mjumbe wa kamati hiyo kwamba aliwakamata wajumbe wenzake watatu wakiomba rushwa kwa viongozi wa Halmashauri ya Handeni.

Katika maelezo yake bungeni, Kafulila aliwataja wabunge wawili kati ya watatu anaowatuhumu kuwa ni Mbunge wa Mbozi Mashariki (CCM), Godfrey Zambi na Mbunge wa Bahi (CCM), Omary Badwel na kwamba taarifa za tukio hilo alikuwa amekwishaziwasilisha kwa Mrema na Spika wa Bunge, Anne Makinda.

Yaliyojiri Lushoto, Handeni

Taarifa ya kamati hiyo ndogo ya LAAC kuhusu Halmashauri za Mkoa wa Tanga inaweka bayana kwamba katika ziara yake wilayani Lushoto Mei 23, mwaka huu kamati hiyo ndogo ilijadili hesabu za halmashauri hiyo na kubaini kuwa kwa miaka mitatu mfululizo, imekuwa ikipata hati zenye shaka za ukaguzi wa CAG.

Miongoni mwa udhaifu mkubwa uliobanishwa ni malipo ya Sh117 milioni ya mishahara kwa watumishi hewa, kiasi cha Sh15 milioni kutumika nje ya bajeti, Sh65 milioni kukusanywa kwa kutumia stakabadhi za kughushi, uchache wa fedha zilizopelekwa katika shule za msingi ikilinganishwa na kiasi kilichotolewa na Hazina na kutopelekwa kwa Sh75 milioni ambazo ni ruzuku ya lazima ya Serikali Kuu kwa ajili ya maendeleo vijijini.

Wilayani Handeni, kamati hiyo pia ilibaini udhaifu kadhaa ikiwa ni pamoja na kiasi cha Sh18 milioni cha malipo ya mishahara kwa watumishi hewa, kutoonekana kwa lambo la kunyweshea maji mifugo lililodaiwa kujengwa eneo la Madebe kwa gharama ya Sh35.5 milioni na kutokuwapo kwa vitasa pia sakafu kubomoka katika soko la Sindeni ambalo limegharimu Sh24.5 milioni.

Udhaifu mwingine katika Halmashauri ya Handeni ni kutopeleka vijijini kiasi cha Sh105 milioni kwa ajili ya kufidia kodi zilizofutwa na matumizi ya mabati 466 ambayo yanadaiwa kutumika kujenga vyumba vinne tu vya madarasa ya Shule ya Sekondari Segera.

Hatua zilizochukuliwa

Pamoja na udhaifu huo, Kamati hiyo ndogo inatoa mapendekezo ambayo mmoja wa wajumbe wake anayaita kuwa ni "dhaifu" yasiyolingana na uzito wa kasoro zilizobainishwa katika Halmashauri ya Handeni.

Mapendekezo hayo ni matatu ambayo yanaitaka ofisi ya ukaguzi ya halmashauri hiyo kujadiliana kuhusu kufungwa au kutofungwa kwa hoja ya uchakavu wa mali mbalimbali zenye thamani ya Sh520 milioni, halmashauri kuongeza bidii kudai fedha zake kiasi cha Sh133.3 milioni katika taasisi tatu tofauti na kuitaka kuweka wazi kwa madiwani na wananchi gharama zitakazotumika kujenga Bwawa la Kidereko.

"Unaona! Hii ina maanisha nini? Taarifa haisemi kitu kuhusu malipo ya watumishi hewa, wala lambo ambalo halikuonekana, wala haimwajibishi mtu yeyote hata kwa kumpa barua ya onyo. Hapa lazima kuna kitu si bure," alisema mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo ambaye alisema hakwenda Tanga wala Pwani kwa kuwa alipata dharura wakati wa ziara hizo.

Lakini, kwa upande wa Lushoto, tofauti na Handeni, kamati hiyo ilitaka ipatiwe majina ya watumishi hewa waliolipwa mishahara husika, nyaraka za fedha na taarifa za kibenki (bank statements) pia kuagiza Mkurugenzi Mtendaji apewe barua ya onyo na mamlaka yake ya kinidhamu kutokana na uzembe uliosababisha halmashauri yake kupata hati yenye mashaka.

Pia kamati hiyo iliagiza Halmashari ya Lushoto kupeleka mara moja fedha za maendeleo vijijini ili kufidia kodi zilizofutwa na kuhakikisha makato ya malipo ya pensheni yanapelekwa katika mamlaka husika.

Makundi ya wabunge

Kwa mujibu wa muhtasari wa kumbukumbu husika, kamati ndogo iliyokuwa mkoani Tanga ilikuwa na wabunge ambao ni Mrema, Kafulila, Badwel, Zambi, Mbunge wa Kondoa Kaskazini (CCM), Zabein Mhita na Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Susan Kiwanga.

Wengine ni Katibu wa Kamati hiyo, Mswige Dickson Aswile, Mwakilishi wa Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesebu za Serikali (CAG), Denis Mbilinyi na Mary Assey ambaye alikuwa katika msafara wa wabunge hao akimwakilisha Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga (RAS). Kwa mujibu wa toleo la 10 la kitabu cha orodha ya wabunge cha Juni mwaka huu, LAAC ina wajumbe 17.

Mbali na wajumbe waliokwenda Tanga, wengine katika Kamati hiyo ni Makamu Mwenyekiti wa LAAC ambaye pia ni Mbunge wa Kinondoni (CCM), Iddi Azzan, Riziki Lulida (Viti Maalumu, CCM), Subira Mgalu (Viti Maalumu, CCM), Hasnain Mohamed Murji (Mtwara Mjini, CCM), Abdul Mteketa (Kilombero, CCM), Tauhida Nyimbo (Viti Maalumu, CCM), Joseph Selasini (Rombo, Chadema) na Kurthumu Mchuchuli (Viti Maalumu, CUF).

Kwa mujibu wa kitabu hicho, makatibu wengine wa kamati hiyo mbali na Aswile ni Edwin Tongora na Chipanda Chilemeji. Hata hivyo, taarifa ya ziara ya kamati ndogo ya LAAC iliyofanya ziara mkoani Pwani haikuweka bayana majina ya wajumbe waliokuwa katika msafara mkoani humo.

LAAC ni kamati ambayo ilijizolea sifa nyingi kwa jinsi ilivyoanza kazi yake kwa kasi na kuwachukulia hatua watendaji wa halmashauri kadhaa nchini ambao walithibitika kuwa dhaifu katika usimamizi wa rasilimali za maeneo yao ya kazi kiasi kwamba baadhi yao walikatwa asilimia 15 ya mishahara yao kama adhabu mojawapo.

Tuhuma za rushwa

Mbali na tuhuma zilizotolewa na Kafulila kwa wajumbe waliokuwa ziarani Tanga, pia zimetolewa tuhuma mpya kwa baadhi ya wajumbe wa kamati ndogo iliyokuwa mkoani Pwani ambako inadaiwa kuwa kiongozi wa kamati hiyo, Azzan alikuwa akikumbana na upinzani mkali pale alipokuwa akijaribu kuhoji baadhi ya mambo katika halmashauri husika.

Habari zaidi zinadai kwamba hata kamati iliyokwenda Pwani baadhi ya wajumbe wake wanatuhumiwa kuomba rushwa kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, ambaye baada ya kumpigia simu alitoa taarifa kwa kiongozi wa timu hiyo, Azzan.

Hali hiyo inadaiwa kuitafuna Kamati hiyo kiasi kwamba imeshindwa kukutana tangu kuanza kwa mkutano wa nne wa Bunge la bajeti, licha ya Mwenyekiti Mrema kuitisha vikao mara tatu kwa nyakati tofauti.

Mrema aliliambia Mwananchi kuwa atamweleleza Spika kuhusu hali ya kamati yake ili kupata mwongozo wa nini kinachotakiwa kufanywa. Vikao vilivyokwama ni vile vilivyotishwa Juni 16, Juni 20 na Julai 19, mwaka huu na ajenda saba zilizokuwa zimepangwa kujadiliwa zimeendelea kuwekwa kiporo.

Kikao cha Julai 19, kilikuwa kimepanga pamoja na mambo mengine, kupitia kumbukumbu ya yaliyojiri katika ziara za Tanga na Pwani, makubaliano ya kujadili taarifa za hesabu za baadhi ya halmashauri wakati kamati ikiwa bungeni, makubaliano kuhusu mwaka wa hesabu (2008/09) au 2009/10) zitakazoendelea kujadiliwa katika kipindi kijacho na Taarifa ya Katibu wa Kamati kuhusu barua kutoka kwenye halmashauri kwenda kwa Katibu wa Bunge.

Mrema katika mazungumzo yake na gazeti hili alisema: "Nikiwaita akija Kafulila baadhi yao hawaji, lakini Kafulila asipokuwepo, wengine utawaona wamefika na hapo unakuwa huwezi kuwa na kikao kinachoweza kufanya uamuzi kwa manufaa ya nchi yetu".

Habari zaidi zinadai kwamba, tuhuma za Kafulila bungeni dhidi ya Zambi na Badwel zinawatisha hata baadhi ya wale waliokuwa katika kamati ya mkoani Pwani kwani wanahofu kwamba huenda nao wakaanikwa ndani ya kikao cha kamati hiyo ya LAAC. Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo aanasema ili kuinusuru kamati hiyo, ipo haja ya kuvunjwa na kuundwa upya kwani hivi sasa ni kama imesambaratika kwani wajumbe husika hawaaminiani.

"Ni bora ikaundwa upya, kazi hazifanyiki na sasa tuna viporo kwa sababu hesabu za mwaka 2009/2010 bado kabisa hatujazigusa na mwezi Aprili mwakani lazima tuwasilishe taarifa bungeni, sasa tutawasilisha nini kama kazi hazifanyiki?" Alihoji mjumbe huyo.

Kanuni za Bunge

Pamoja na Kanuni ya 114 (3) kusema kwamba kamati zinaweza kukutana kila itakapotakiwa kufanya hivyo na Spika, Naibu Spika au Mwenyekiti wa Kamati husika kwa idhini ya Spika, kanuni hizo haziweki wazi hatua zitakazochukuliwa ikiwa wajumbe wa kamati watashindwa kukutana kama ilivyotokea kwa LAAC.

Ama kanuni za 113 (6) na (7) zinaeleza kuwa ujumbe wa mbunge katika kamati unaweza kukoma ifikapo mwishoni mwa mkutano wa kumi wa uhai wa bunge, ikimaanisha kuwa hakuna mbunge anayeweza kuodoka katika kamati yake ya sasa hadi mkutano wa kumi utakapofikia ukomo.

Huu ni Mkutano wa Nne wa Bunge la 10 na Mkutano wa 10 unatarajiwa kufanyika ifikapo Oktoba 2012, wakati kamati za kudumu za bunge zitakapopangwa upya.

Kwa maana hiyo ni vigumu kwa sasa LAAC kufanyiwa marekebisho kwa mujibu wa kanuni au kuundwa upya, isipokuwa Spika aamue kutumia vifungu vingine vya kanuni vinavyompa mamlaka ya kifanya jambo kadri anavyoona yafaa.

Madiwani Chadema 'ngangari'

Moses Mashalla, Arusha
MADIWANI watatu wa Chadema waliotakiwa kujiuzulu nyadhifa zao katika Halmashauri ya Manispaa ya Arusha kufikia saa 7:02 mchana jana, wamegoma kufanya hivyo na badala yake wameutaka uongozi wa taifa wa chama hicho kuwasafisha kwa kuwataka radhi.

Kauli hiyo ya madiwani hao akiwamo Naibu Meya wa Jiji la Arusha, Estomi Mallah imekuja siku chache baada ya kuvuja kwa ripoti ya kamati iliyoundwa na Chadema kuchunguza mwafaka wa madiwani wake, wa CCM na TLP katika kumpata Meya wa jiji hilo ikibainisha kuwa hakukuwa na tuhuma za rushwa katika mchakato huo.

Badala ya kujiuzulu, madiwani hao wametoa masharti magumu kwa chama hicho, licha ya kutaka kusafishwa, pia wamemtaka Katibu Mkuu, Dk Willibrod Slaa na Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema kuwasafisha kwa kutoa taarifa kwa vyombo vya habari kueleza umma kwamba hawakuhongwa.

Mallah ambaye ni mwenyekiti wa madiwani hao alisema jana kuwa wamekitaka chama chao kuwaomba radhi kupitia vyombo vya habari kwa kuwa ripoti hiyo imebainisha ukweli wa mambo. Alisema taarifa za wao kuhongwa zilizotolewa na uongozi wa chama chao ziliwasababishia usumbufu mkubwa ndani ya jamii zao kiasi cha kufanya baadhi yao kunusurika kupigwa mawe.

Akizungumzia agizo la kujiuzulu nyadhifa ndani ya manispaa hadi kufikia jana saa 7:02, alisema wamepanga kukata rufaa dhidi ya uamuzi huo kwa kuwa hawakutendewa haki. Mallah aliutaka uongozi wa Chadema kutambua misingi ya haki huku akibanisha kuwa migogoro ya ndani kwa ndani huenda ikakipeleka mahali kubaya akisema kama kuna tatizo, linapaswa kutatuliwa kupitia vikao na si vinginevyo.

Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu, Afya na Uchumi ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Elerai (Chadema), John Bayo alikwenda mbali akimtaka Lema kupita katika maeneo yote ya Jiji la Arusha kuwasafisha mbele ya wananchi kutokana na tuhuma alizozitoa kuwa walipokea rushwa.

Chadema kimetofautiana na madiwani hao kwa kile inachoeleza kuwa wamepingana na msimamo wa chama hicho kutotambua mwafaka katika mgogoro wa Meya wa Halmashauri ya Jiji la Arusha.

Chama hicho kikuu cha upinzani nchini kinapinga jinsi muafaka huo ulivyofikiwa kikisema haukufuata misingi ya kisheria ba kwamba ili mwafaka upatikane mambo kadhaa yalipaswa kujadiliwa kwa pamoja ikiwa ni pamoja na kufutwa kwa kesi iliyofunguliwa dhidi ya viongozi wa chama hicho kutokana na maandamano yaliyofanyika mapema mwaka huu kupinga matokeo ya uchaguzi wa meya, kulipwa fidia kwa familia za marehemu waliokufa kwenye maandamano hayo na uchaguzi wa meya wa jiji hilo kurudiwa.

Uongozi wa taifa wa chama hicho unaona kwamba kitendo cha madiwani hao kukubali nyadhifa ndani ya Baraza la Madiwani wa Jiji la Arusha kabla mambo hayo hayajatekelezwa, kimetafsiriwa na Kamati Kuu ya Chama hicho kuwa ni usaliti uliotokana na rushwa.

Wahudhuria kikao cha halmashauri ya jiji

Licha ya madiwani hao kupuuza agizo hilo la makao makuu ya Chadema, jana walihudhuria kikao cha Baraza la Madiwani kilichokuwa kikifanyika kwenye Ukumbi wa Halmashauri ya Manispaa ya Arusha kama kawaida huku baadhi yao wakisema sasa wameamua kufanya kazi ya kuwatumikia wananchi waliowachagua ili kuwaletea maendeleo na kuweka pembeni tofauti za kisiasa.

Dk Slaa alipoulizwa jana kuhusu msimamo wa madiwani hao, alisema Katiba ya Chadema itachukua nafasi yake katika kuamua suala hilo akisema asingependa kuibua malumbano katika suala hilo wala kutunishiana misuli. Alisema diwani yoyote anayeona kwamba hakutendewa haki ana haki ya kwenda mahakamani.

"Katiba ya Chadema itakwenda kufanya kazi, kamati kuu iliwataka wajiuzulu mara moja kama wamekataa sasa katiba itachukua mkondo wake na yoyote anayeona alichafuliwa yuko tayari kwenda mahakamani," alisema.

Mgogoro huo wa umeya Arusha ulisababisha mauaji ya watu watatu katika maandamano yaliyofanyika Aprili mwaka huu, mmoja wao akiwa ni raia wa Kenya baada ya Chadema kuamua kuandamana kwa nguvu bila kibali cha polisi.
SOURCE:Mwananchi

Friday, July 15, 2011

Lowassa: Nimeshtushwa


Leon Bahati, Dodoma, Ramadhan Semtawa, Dar
WAKATI uamuzi wa Rostam Aziz kung'atuka ubunge wa Igunga na ujumbe wa Halmashauri Kuu (Nec) ndani ya chama chake cha CCM ukiibua gumzo kubwa karibu kila kona nchini, mshirika wake mkubwa kisiasa, Edward Lowassa ambaye ni Mbunge wa Monduli ameeleza kushtushwa na tukio hilo.Juzi, Rostam, mmoja wa watu muhimu ndani ya CCM aliyeshiriki vyema katika mtandao uliomwingiza madarakani Rais Jakaya Kikwete mwaka 2005, alitangaza uamuzi mzito wa kung'atuka siasa akipinga kile alichokiita siasa uchwara za baadhi ya viongozi wake.

Uamuzi huo mzito wa Rostam uliibua kwikwi na vilio kutoka kwa wapigakura jimboni kwake Igunga, wakiwamo wale waliomchagua kwa vipindi vitatu mfululizo tangu mwaka 1994 ulipofanyika uchaguzi mdogo kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Charles Kabeho. Jana, Lowassa alisema: "Kwa kweli nimeshtushwa, nimesikitishwa...kilichonishtua zaidi ni vilio. Namna wananchi wa Igunga walivyokuwa wanalia na kusikitika."

Hata hivyo, Lowassa ambaye naye amekuwa akitajwa katika orodha ya watu watatu wanaopaswa kuachia nafasi zao za uongozi CCM katika kile kinachoitwa chama kujivua gamba, alipoulizwa kuhusu taarifa za yeye kufuata njia ya mshirika wake huyo alijibu: "Siku ikifika nitatoa uamuzi na nitajibu wakati ukifika."

Lowassa alikuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari katika Viwanja vya Bunge mjini Dodoma, kuhusu alivyopokea uamuzi huo wa Rostam na kama yuko tayari kufuata mfano na njia hiyo ya kujiuzulu nyadhifa zote ndani ya CCM.

Lakini, juzi Rostam aliweka bayana kwamba uamuzi wake wa kujiuzulu hautokani na shinikizo lolote ikiwamo kile kinachoitwa mpango wa kujivua gamba, bali aliufanya uamuzi huo kuepuka kuathiri biashara zake kutokana na kuchafuliwa na siasa uchwara akieleza kuwa yeye ni mfanyabiashara wa kimataifa, lakini akaahidi kuendelea kuwa mwanachama mtiifu wa CCM.

Hata hivyo, Lowassa jana hakutaka kufafanua kuhusu kauli yake hiyo ya "Nitajibu wakati ukifika," ingawa alionyesha tabasamu wakati akiulizwa na kujibu swali hilo la iwapo atafuata nyayo za Rostam au la.
Mshirika wao mwingine, Andrew Chenge, jana alivumishiwa kuandaa mkutano na waandishi wa habari ili naye atangaze uamuzi wa kujiuzulu nafasi zake zote kama hatua ya kutekeleza azimio la Nec la kujivua gamba.

Lakini, alipotafutwa kwa simu na kuulizwa kuhusu taarifa za yeye kutaka kujiuzulu, Chenge alijibu kwa kifupi kuwa alikuwa Uingereza, kitu kilichothibitisha kuwa hakukuwa na mpango huo wa kujiuzulu huku akisisitiza: "Mimi niko nje ya nchi, nipo Uingereza."

Hivi karibuni, Chenge, Mbunge wa Bariadi Magharibi, maarufu kama Mzee wa Vijisenti, aliwahi kuliambia gazeti hili: "Sijui kama mimi ni gamba CCM," huku akisisitiza kwamba anaheshimu taratibu za chama na asingeweza kukurupuka na kuanza kuzungumza mambo ya chama nje ya utaratibu.

Chenge alisema chama kina utaratibu wake wa kufanya maamuzi, hivyo kuanza kutoka nje ya taratibu na kuzungumzia mambo ya ndani ya chama isingekuwa rahisi kwake kwani anaheshimu taratibu zilizopo.

..Sendeka asifu ujasiri wa Rostam
Kwa upande wake, Mbunge wa Simanjiro (CCM), Christopher Ole-Sendeka, ambaye amekuwa akijipambanua kama mpambanaji wa ufisadi, alisema kujivua kofia zote alizokuwa nazo Rostam ni kitendo cha kuletea afya chama tawala.Sendeka alifafanua kwamba kuwapo kwa vigogo wanaotuhumiwa kwa rushwa ndani ya CCM ni sawa na mtu anayeugua na ili apone lazima waondoke ili chama kipate afya njema.

Alisema kutokana na sababu hiyo, anamuunga mkono Rostam kwa uamuzi wake aliochukua wa kutii uamuzi wa chama wa kujivua gamba, kwani ni hatua moja ya kukiboresha chama na kuongeza: "Unaposhauriwa kwa afya ya chama chako na ukakubali ni uamuzi wa kijasiri."

Hata hivyo, alionya kwamba mkakati huo wa kujivua gamba ni zaidi ya vigogo watatu ambao wamekuwa wakitajwa mara kwa mara.Sendeka alisema wote wakifuata mkondo wa Rostam, chama kitajijengea taswira nzuri ya kupendwa na watu ambao tayari wameanza kukata tamaa kutokana na kuona haya kutokana na tuhuma zinazowahusu.

Kuhusu wale ambao bado hawajatekeleza hilo, ole-Sendeka alisema: "Cheo ni dhamana, uongozi ni utumishi, kama wale waliokupa dhamana wanakushauri uondoke, huna haja ya kubishana, tekeleza."Naye Ally Mohamed (Nkasi Kaskazini-CCM), alisema amefurahishwa na hatua ambayo Rostam ameichukua kwa lengo la kusafisha chama.

Lakini, akasema ni wakati mwafaka wa kuhakikisha CCM inasafishika mbele ya Watanzania kwa sababu, kuwapo kwa watuhumiwa hao wa ufisadi wanaozungumzwa mara kwa mara, kulionekana kuchafua chama chote."Sasa ni wakati wengine nao wachukue uamuzi kama huo. Tunajua wako wengi, waondoke chama kiimarike," alisema Mohamed.

Tundu Lisu azungumzia uamuzi wa Rostam
Tundu Lissu (Singida Mashariki-Chadema), alisema bado gamba la CCM halijavulika kwa sababu Rostam ni mmoja wa watuhumiwa 11, ambao walitajwa na Chadema kwenye orodha ya mafisadi, Mwembeyanga, Temeke mwaka 2007.

"Bado kumi," alisema Lissu huku akijigamba kuwa mafanikio hayo ni juhudi zilizofanywa na Chadema ili kulinda rasilimali za Watanzania ili zitumike vizuri.

Kuhusu kauli ya Rostam kuwa amejing'oa kwenye nyadhifa zake kutokana na "siasa uchwara", Lissu alijibu: "Kama kweli siasa uchwara ndizo zimemwondoa Rostam, basi ndizo zinazofaa kuendelezwa hapa nchini."

 Ingawa Rostam alikataa kuhusisha uamuzi wake na kujivua gamba, tangu kikao cha Nec cha Aprili, Sekretarieti mpya ya CCM imekuwa ikitangazia umma orodha ya makada wake watatu ambao wanapaswa kujiuzulu ili kuleta kile inachokiita heshima kwa chama na kukisafisha.

Uamuzi wa Rostam kung'atuka watikisa nchi


Waandishi Wetu
TUKIO la Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz kuachia nyadhifa zote za uongozi ndani ya CCM, limepokelewa kwa hisia tofauti baada ya watu wa kada mbalimbali kutoa maoni tofauti huku baadhi yao wakimsifu na wengine kumponda.

Hata hivyo, chama hicho tawala kimeeleza kuwa hakijapata taarifa rasmi za uamuzi huo wa Rostam ingawa yeye alisema jana kuwa, barua yake ya kujiuzulu aliikabidhi kwa mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete.
Baadhi ya wanasiasa wamemponda mwanasiasa huyo, huku wasomi na baadhi ya viongozi wa dini wakisema kuwa hatua yake hiyo ni sahihi katika mwenendo wa sasa wa siasa ndani ya chama hicho.

Kwa mujibu wa wasomi na viongozi hao wa dini, hatua hiyo ya Rostam imeelezwa kuwa ni mfano kwa viongozi wengine wa chama na Serikali yake wanaojiona kuwa wanaelemewa na tuhuma mbalimbali.
Mwanasheria maarufu nchini, Profesa Abdallah Safari alisema kuwa, uamuzi huo ni ujumbe kwa viongozi wengine wa CCM wanaonyoshewa kidole kila kukicha.

“Kwa maoni yangu, uamuzi huo umemsaidia Rais Kikwete kwani kati ya watu waliokuwa wakinyoshewa sana vidole, mmoja wao ameamua kujiondoa, kwa kweli amemwondolea mtihani, lakini pia itasaidia chama ambacho nacho kilikuwa kikinyooshewa sana vidole,” alisema Profesa Safari.Hata hivyo, alisema hatua hiyo ya viongozi kujivua nyadhifa zao haitatosha kukisafisha chama hicho dhidi ya maovu.

“Kuna ubadhirifu mwingi ambao unatakiwa ufanyiwe kazi, mambo mengine kama EPA na Richmond hayawezi kumalizwa kwa watu kujivua nyadhifa zao,” alisema msomi huyo.Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Bashiru Ally, alisema hotuba ya Rostam aliyoisoma mbele ya wazee wa Igunga, inaonyesha kwamba amejiuzulu kwa shingo upande.

“Nimesoma hotuba yake yote, lakini inaonyesha wazi kwamba ameachia nyadhifa ndani ya chama hicho ikiwa ni kutekeleza kauli ya CCM ya kujivua gamba, inaonyesha kwamba amechukua uamuzi huo kwa shingo upande,” alisema Bashiru,

CCM: Hatujapata barua yake
Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama, alilieleza Mwananchi jana kuwa mpaka wakati huo chama hicho hakikuwa kimepokea taarifa hizo rasmi na kwamba hata wao walizipata kupitia vyombo vya habari jana, hivyo hawapo katika nafasi nzuri ya kutoa tamko linaloweza kuwa msimamo chama.

"Hata sisi (CCM) tumepata taarifa hizo kupitia vyombo vya habari kama nyinyi, hivyo hatuwezi kutoa msimamo wa chama kwa sasa," alisema Mukama.

Rostam: Barua yangu ipo kwa Mwenyekiti
Hata hivyo, Rostam mwenyewe akizungumza na Mwananchi jana, alisema tayari alishamwandikia barua Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete kuhusu uamuzi wake huo.

Alifafanua kwamba, CCM ndiyo yenye mamlaka na inayopaswa kulieleza Bunge kwamba kiti hicho kiko wazi.
Alisema tangu kutangaza uamuzi huo, hadi jana mchana tayari alikuwa amepata salamu na ujumbe mfupi (sms) kutoka kwa wanachama 11,872, wa CCM ambao walimpongeza kutokana na hotuba yake.

Kwa mujibu wa Rostam, wanachama hao walikubaliana naye kuhusu siasa uchwara zinazoendeshwa na chama hicho katika kipindi hiki, hadi kuamua kuchukua uamuzi huo.

Rostam alisema mbali na ujumbe wa simu, pia alipata simu kutoka kwa wanaCCM wengi Kanda ya Ziwa ambapo waliunga mkono hotuba yake. Inaelezwa kuwa Rostam ana ngome kubwa ya wafuasi kwenye mikoa ya Kigoma, Mara, Mwanza, Tabora na Shinyanga.

Nape akwepa
Kwa upande wake, Katibu wa Idara ya Itikadi ya Uenezi, Nape Nnauye, alisema hakuwa na la kusema juu ya tuhuma ambazo ametupiwa na Rostam kupitia hotuba yake ya kujivua nyadhifa zake.

Wakati akizungumza na aliowaita wazee wake juzi, Rostam alituhumu Sekretarieti ya CCM kwamba ilieneza kwa kupotosha nia njema ya Mwenyekiti wao (Rais Kikwete) katika dhana ya chama hicho kujivua gamba akisema kuwa, ilienezwa kwa tafsiri na mwelekeo tofauti na ule wa awali.

"Wajumbe wawili wa Sekretarieti, Naibu Katibu Mkuu (Tanzania Bara), John Chiligati na Katibu wa Idara ya Uenezi, Nape Nnauye, walisikika wakitangaza kwamba Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) ilifikia uamuzi wa kuwapa siku 90 wale walioitwa watuhumiwa wa ufisadi kujitoa katika nafasi zao za uongozi vinginevyo watafukuzwa na chama," inaeleza sehemu ya hotuba hiyo ya Rostam.

Hotuba hiyo ilieleza kuwa viongozi hao walikaririwa na vyombo vya habari wakieleza kuwa majina ya watuhumiwa hao yalikuwa yakifahamika kutokana na kuhusishwa katika kashfa za Richmond, EPA na ununuzi wa rada na hatimaye walitaja majina ya wanasiasa watatu kuwa ndiyo ambao walilengwa na uamuzi huo.

Rostam Aziz alisema kuwa jina lake kutajwa katika orodha ya watuhumiwa hao ni ufinyanzi wa porojo na fitina za kisiasa, ambao ulimshangaza, kutokana na namna uamuzi halisi wa Nec, hususan kuhusu 'kujivua gamba'¯ ulivyopindishwa na wajanja wachache kwa maslahi binafsi ya kikundi fulani cha watu.

Alisema mshtuko na mshangao wake umejikita katika viongozi wa chama hicho alichotumikia kwa bidii na uaminifu mkubwa, kufanya juhudi kubwa hata kufikia hatua ya kukivisha kikao alichokiita kitukufu cha Nec uamuzi ambao msingi wa hoja zake ni vita vya kimakundi ya siasa ndani ya CCM, propaganda za vyama vya siasa vya upinzani na vyombo vya habari kwa upande mwingine.

Katika hotuba yake, Rostam alieleza kushangazwa na kushtushwa kwake na ujasiri ambao viongozi wa Sekretarieti mpya ya CCM wamekuwa nao, kiasi cha kutaja jina lake kwa kulihusisha na kile wanachokiita ufisadi ambao hata kimsingi ushahidi wa wazi umethibitisha kuwa ni porojo za kisiasa zinazotokana na makovu na matarajio ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 na ule ujao wa 2015.

Mkoani Kilimanjaro
Askofu Msaidizi wa Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Frederick Shoo, alisema hakuamini aliposikia taarifa hizo, lakini baadaye aliamini na kusema mbunge huyo amesoma alama za nyakati.
“Ni uamuzi mgumu aliouchukua, lakini ulistahili kwa mazingira ya siasa za Tanzania na amesoma vizuri alama za nyakati…na wengine wote wanaotajwa kuwa na tuhuma nao wafuate nyayo hata kama hazijathibitishwa,”alisema Shoo.

Mkurugenzi wa Huduma za Ushauri, Chuo Kikuu Kishiriki cha Ushirika na Biashara Moshi (MUCCoBS), Michael Tiruhungwa, alisema Rostam angewatendea haki Watanzania kama angejielekeza zaidi kwenye tuhuma anazohusishwa nazo.

Naye Mtaalamu Mshauri wa Huduma za Biashara, Akwiline Kinabo, alisema kujiuzulu kwa Rostam ni mwanzo tu na kama kweli CCM imedhamiria kujivua gamba, basi Watanzania watarajie mengi makubwa zaidi ya kujiuzulu.

Kutoka Mwanza
Katibu wa Chadema Mkoa wa Mwanza, Wilson Mushumbusi, alisema uamuzi wa Rostam kujiuzulu umetokana na wakati mgumu wa kisiasa alionao.
Mushumbusi alifafanua kwamba mbunge huyo amekuwa akituhumiwa kwa kashfa nyingi, kujiuzulu kwake ni mwanzo wa mafanikio ya Chadema juu ya madai ya ufisadi ambayo yanamkabili.

Katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UV-CCM) Mkoa wa Mwanza, Josephat Ngolangwa alisema Rostam ameonyesha ukomavu wa kisiasa na uamuzi wake umekinusuru chama.

Alifafanua kwamba, hatua hiyo inadhihirisha Rostam ni muumini wa dhati wa chama chake na kuwataka wengine waliotuhumiwa ndani ya chama na hata katika Serikali, wafuate nyayo za Rostam ili kurejesha imani kwa chama.
Alisema CCM kama taasisi ya kisiasa inafanya uamuzi kutokana na vikao na haya yote yanayotendeka ni uamuzi wa vikao vya chama wa kuwataka viongozi wote kusimamia uamuzi wa vikao vya chama ngazi ya juu.

Kwa msisitizo, alisema kwa sasa viongozi wana kazi kubwa ya kuimarisha chama na siyo wakati wa kujadili nani atakuwa rais katika kipindi kijacho cha mwaka 2015 kwa kusema kuwa 2015 ni mbali sana.

Mkoani Tanga
Nako mkoani Tanga watu wamepokea uamuzi huo wa Mbunge wa Igunga kwa mitazamo tofauti, huku wengine wakitaka mapacha wenzake ambao wamekuwa wakitajwa na viongozi wa CCM kuhusika na tuhuma za ufisadi wafuate nyayo zake.

Wasomi na wanasiasa waliozungumza na gazeti hili jana walisema kung’atuka kwa Rostam Aziz ni tukio ambalo lilitarajiwa.

Mkereketwa wa CCM, Tarafa ya Mlalo, Wilayani Lushoto, Zahabu Mjata alisema kitendo cha Rostam kuachia ngazi ni cha kiungwana na kwa hiyo hastahili kusakamwa kama inavyofanywa na baadhi ya watu.

Mtei amshika pabaya Wassira

Moses Mashalla, Arusha
MUASISI wa Chadema hapa nchini, Edwin Mtei "amemshika pabaya" Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais (mahusiano na uratibu) ,Stephen Wassira akitaka ajiuzulu kwa kulala bungeni.

Pamoja na kupongeza picha ilivyotoka gazetini, alisema kitendo cha kigogo huyo kuuchapa usingizi bungeni kimedhibitisha jinsi Serikali ya Rais Jakaya Kikwete isivyokuwa makini na kumtaka Wassira ajiuzulu mara moja.

Mtei,alitoa kauli hiyo siku moja kupita baada ya wakazi wa Mkoa wa Kilimanjaro wakiwamo wasomi kuunga mkono hatua ya gazeti hili kumpiga picha waziri huyo akiwa amelala bungeni huku wakisema kuwa ni sahihi na kubeza kauli ya waziri huyo kuwa kitendo hicho ni uchochezi.

Akizungumza na gazeti hili, Mtei alisema kitendo cha waziri huyo kusinzia bungeni kimemdhalilisha yeye mwenyewe pamoja na Serikali ya Rais Kikwete na kusisitiza kwamba Serikali haiko makini kutatua kero za umma.

"Kitendo cha Wassira kusinzia bungeni kimetuonyesha ni jinsi gani Serikali ya CCM isivyokuwa makini kutatua kero za umma,amejidhalilisha
kwanza yeye mwenyewe, lakini pia wananchi anakotoka na Serikali nzima mimi namshauri aachie ngazi tu"alisema Mtei.

Alisema mara kwa mara chama chao kimekuwa kikiilaumu Serikali kwa kutokuwa makini na kero zinazoligusa taifa hivyo kitendo cha waziri huyo kuuchapa usingizi bungeni kimetoa majibu ya madai yao.

Hatahivyo, alipuuza vikali hoja ya Wassira kuwa kitendo cha gazeti hilo kumpiga picha akiwa amelala kuwa ni uchochezi huku akisema kuwa
kama alikuwa mgonjwa angeenda kupumzika nyumbani kwake na sio kusinzia bungeni.

Mtei,ambaye pia aliwahi kuwa gavana wa Benki Kuu hapa nchini alilipongeza gazeti la Mwananchi kwa kuwafichua wabunge wanaolala bungeni huku akisema kwamba kamwe lisirudi nyuma katika kusimamia maadili ya taaluma ya habari.

"Mwananchi lisirudi nyuma, mnatusaidia sana kuwafichua viongozi wanaolala bungeni bila nyie sisi tusingejua endeleeni na msiogope"alisisitiza Mtei.

Pia alizungumzia kero ya mgao wa umeme uliolikumba taifa na kusema kuwa Serikali ya Rais Kikwete imeshindwa kutatua kero za taifa hali ambayo imesababisha taifa kuendelea kuwa maskini.

Alisema kuwa kero ya mgao wa umeme ni mzigo mkubwa wa Watanzania ambao hauvumiliki huku akionya ya kuwa endapo hali hiyo isipotatuliwa mara moja huenda nchi ikaingia katika matatizo makubwa ikiwa ni pamoja na vijana kukosa ajira,viwanda kufungwa kwa kushindwa kufanya kazi na uchumi kuporomoka.

SOUCE:MWANANCHI

MZIMU WA SERIKALI TATU WARUDI BUNGENI

Leon Bahati, Dodoma
MTAZAMO tofauti miongoni mwa wabunge umeendelea kuwa chachu ya kutaka kuvunjwa kwa muungano wa Tanzania.Hali hii imejionyesha wazi wiki hii katika mkutano wa Bunge unaoendelea mjini Dodoma baada ya wabunge kuvutana kuhusu hatima yake, huku baadhi yao wakitaka uvunjwe na kuundwa upya na wengine kuutetea.


Chanzo cha mvutano huo ni kufutia baadhi ya wabunge kutoka Zanzibar kuubeza na kuonyesha wazi kuwa Tanzania bara inanufaika zaidi kuliko visiwani.

Hoja hii si tu kwamba iliwakoroga wabunge wa bara, bali pia wananchi walioisikia wamekuwa wakihoji sababu za wabunge hao kuubeza muungano kana kwamba hauwasaidii.

Kauli tata kuhusu muungano ambazo kwa ujumla zinadhoofisha uhusiano baina ya pande hizo mbili, ulianza muda mrefu hasa baada ya nchi kuingia katika mfumo wa vyama vingi vya saisa na unaendelea kukua kadiri muda unavyosonga mbele huku Serikali ikifanya jitihada za kuunusuru.

Katika mvutano ulioibika bungeni wiki hii, wabunge wa Chadema na baadhi wa Chama cha Wananchi (CUF), walioonekana dhahiri kutaka muundo wa sasa wa Muungano huo uvunjwe na kuundwa mwingine wenye serikali tatu; Tanganyika, Zanzibar na Serikali ya Muungano.

Hata hivyo, mfumo huo umekuwa ukipingwa kila mara kwa vile ni sawa na kumwondole madaraka na nguvu Rais wa shirikisho kwa vile hatakuwa na uwezo kuingilia mambo ya ndani ya serikali ya mbili zitakaozoundwa.Hata hivyo, wakati wabunge hao wakitetea hoja hiyo, wengine kutoka Chama tawala CCM, na baadhi ya mawaziri akiwamo Samuel Sitta wa Afrika Mashairiki, walisimama kudete kuutetea.

Hoja za wabunge
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, alishutumu tabia ya viongozi waliopo madarakani kuficha ukweli juu ya suala zima la muungano akiweka bayana kuwa sasa ni wakati mwafaka Watanzania wakajadili hatima ya Muungano huo.

Akitumia vitabu vya watu mashuhuri kama vile Rais wa Pili wa Zanzibar, Aboud Jumbe na Profesa Issa Shivji, Lisu
alisema matatizo na kero nyingi zinatokana na baadhi ya mambo kutowekwa wazi.Alitaja baadhi ya mambo aliyosema siri kuwa ni juu ya Mapinduzi ya Zanzibar na lengo hasa lililolazimu uwepo wa muungano huo.

Mambo mengine alisema ni kuingizwa kinyemela kwenye katika ya Tanzania vipengele kuanzia cha 11 hadi 22.Halima Mdee wa Kawe, alisema kero za muungano zimekuwa hazitatuliwi kutokana na waziri mwenye mamlaka ya muungano kupuuzwa na viongozi wenye mamlaka ya juu katika kuamua kusu suala hilo.

Aliwataja viongozi hao ambao alidai hawana muda wa kutulia ili kutafuta ufumbuzi wa kero hizo kutokana na kuwa na kazi nyingi kuwa ni Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar.

Alilalamika kuwa kutokana na hali hiyo ni kero sita tu zimetatuliwa, huku saba ambazo ni za msingi, zikiendelea kupigwa danadana.Miongoni mwa kero hizo sugu, alizitaja kuwa ni suala la mafuta, ushiriki wa Afrika Mashariki na suala sahihi za waanzilishi wa Muungano huo.

"Suala la kodi mbili ni kiini macho na kwamba wananchi wengi wamekuwa wakiathirika kutokana na tatizo hilo," alieza Mdee ambaye alipendekeza Katiba ijayo kuwa na mwanga wa kutatua kero za muungano.

Mohamed Amour Chomboh (Magomeni) alitamba kuwa yeye ni miongoni mwa watu wachache walioshuhudia Mapinduzi ya Zanzibar yalivyofanyika na anatambua ni muhimu kuenziwa.Alisema anaona kuna umuhimu wa muungano huo kuendelea kudumu lakini, akaasa kuwa kero zake zimekuwa ni tishio kubwa hasa kwa maslahi ya Zanzibar.

Alilalamikia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwa ndio moja ya kero ambazo zinaweza kusababisha Wazanzibari waje juu na hata kutaka kuvunja Muungano.Alisema Zanzibar inategemea zaidi bishara kwa ajili ya kuimarisha uchumi wake na kwamba TRA ndiyo imekuwa ikisababisha biashara kudorora visiwani humo.

Waziri atwishwa mzigo
Jaddi Sumail Jaddi (Mkwajuni-CCM) alisema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Hassan Suluhu ,ambaye ni Mzanzibar alikabidhiwa nafasi hiyo kama mtego wa kumbebesha lawama za kero za Muungano ambazo zinalalamikiwa na Wazanzibar.

"Ndugu yangu Samia ni mchawi aliyepewa mtoto amlee akimnyonga, alamumiwe yeye," alisema Jaddi.
Sitta alisema huo ni upotoshaji na kwamba alipewa kazi hiyo kwa vile Serikali inaamini kwamba ana uwezo wa kuifanya kazi hiyo.

Yalikuwepo malalamiko kwamba Wazanzibar wanaoajiriwa Bara ni wachache, lakini Sitta alipinga akitoa mfano wa wizara yake ina maofisa wakuu wa idara 12 na kati ya hao, wanne ni Wazanzibari.

Sitta awatuliza
Munkali wa wabunge hao ni kama ulizimwa na Sitta ambaye alifanikiwa kubadili kabisa hali ya hewa iliyokuwa inaashirikia kuwa wabunge wengi wanataka Mungano huo uvunjwe.

Akichangia mjadala huo Sitta alisema siku ambayo Watanzania wataamua kuwa na serikali tatu za muungano, itakuwa ndiyo tiketi ya kuuvunja muungano huo.

"Kuunda tena Tanganyika ni kutengeneza mbia mwingine atakayekuwa anashindana na Zanzibar," alisema Sitta.

Alifafanua kuwa hali hiyo itajenga mazingira ya mvutano kwa serikali ya Tanganyika na Zanzibar wa kila mmoja kupigania maslahi yake na Serikali ya Muungano haitakuwa na nguvu kwa sababu uwepo wake utategemea pande hizo mbili.

Alitoa mfano akisema linaweza kujitokeza suala la kuchangia uendeshaji wa Serikali ya Muungano na hapo yanaweza kujitokeza malalamiko kwamba pande zote zigharimie sawa kwa sawa na hapa Zanzibar ndiyo itakayonyanyasika.

Sitta ambaye alikuwa Spika katika Bunge lililopita alionya akisema kama ni mpango wa kuunda serikali tatu ni bora waridhie kabisa muungano usiwepo na serikali zote zijitegemee.

Alitaka ieleweke kwamba wakati inaonekana kuwa Wazanzibar ndio wanaoonekana kulalamika sana wakati huu kwamba wananyimwa maslahi yao lakini ukweli wapo Watanzania Bara ambao nao wanalalamika vivyo hivyo ila nguvu hiyo inapungua kutokana na kuwepo serikali mbili.

Amtetea Nyerere
Kuhusu Baba wa Taifa kuwa dikteta, Sitta alisema kuwa huo ni upuuzi kwa sababu yapo matendo mengi ambayo yanaonyesha hakuwa mlafi wa madaraka na badala yake alipenda haki kwa wananchi wake na bara la Afrika kwa Ujumla.

Alitoa mfano kuwa kama angekuwa dikteta angeweza kuamua kufuta kabisa uwepo wa serikali ya Zanzibar.
"Lakini alikubali iendelee kuwepo serikali ya Zanzibar ndani ya Muungano," alisema Sitta ambaye pia ni mbunge wa Urambo Mashariki.

Katika kuelezea kuwa Karume hakuwa mtu wa kuburuzwa alisema, Tanzania ilipoishiwa akiba ya fedha za kigeni na kwenda kuiomba serikali ya Zanzibar iwapatie kwa sababu wao walikuwa nazo nyingi kutokana na mauzo ya karafuu, alikataa.

Kuhusu suala la picha ya siku ya Muungano kuonekana Mwalimu Nyerere peke yake akichanganya udongo wa Tanganyika na Zanzibar, Sitta alisema ni suala tu la heshima ambalo alipewa kutokana na wadhifa wake wa Rais wa Muungano.

Alifafanua kuwa siku hiyo waliteuliwa watu wawili, mwanauma na Mwanamke, kutoka pande zote kushiriki katika kufanikisha tukio hilo lililoandika historia ya Tanzania.

Hoja nyingine aliyopangua ni ile ya wabunge wengi kueleza kuwa katiba ilibadilishwa ili Rais wa Zanzibar asiwe tene Makamu wa Kwanza wa Rais tofauti na makubaliano ya waasisi wa muungano kwa hofu ya CCM kwamba Rais wa visiwani anaweza kutoka chama cha upinzani.

Sitta alisema ukweli ni kwamba mabadiliko hayo yalitokea baada ya kuona kwamba nafasi hiyo ya pili itaonekana kuwa ni ya Wazanzibari tu, kwa vile serikali ya Zanzibar daima itaongozwa na mzanzibar.

Zanzibar na OIC
Kuhusu suala la kutaka Zanzibar iruhusiwe ijiunge na Jumuia ya Nchi za Kiislamu Duniani (OIC) kwa vile Tanzania imeamua kutofanya hivyo, Sitta alisema tatizo ni kwamba kanuni haziruhusu.

Alisema kwamba OIC ilikataa kufanya hivyo kwa vile sheria zao ni kujenga ushirikiano na serikali ile inayotambuliwa na Umoja wa Mataifa.

Kuhusu kipengele cha kwanza hadi 11 viliundwa kwa makubaliano ya pande zote lakini baadaye kifungu cha 12 hadi 22 vikaingizwa kinyemela, Sitta alisema, sio kweli.


Kwa mujibu wa Sitta vipengele hivyo vilitokana na kuvunjika kwa Jumuia ya Afrika Mashariki 1977 ambapo baadhi ya mambo mengi yaliyokuwa yanasimamiwa na ushirikiano huo yalibaki bila usimamizi.

Alitaja miongoni kuwa ni Shirika la Posta, reli, bandari na ndege ambapo Tanzania Bara ilibidi iyabebe baada ya rais wa Zanzibar kuridhia.

Hata hivyo alisema Tanzania bara ilibeba jukumu hilo kwa gharamna zake bila kuishirikisha Zanzibar hiyo ikawa ni nafuu kwa Wazanzibar kwa sababu faida zake zinaenda pande zote za Muungano.

Kama hiyo haitoshi, Sitta alisema rais wa Zanzibar aliiomba Bara ianzishe pia elimu ya juu kwa sababu isingeweza kufanya hivyo kutokana na uwezo wa kifedha.

Akipinga malalamiko kwamba Zanzibar haina uwakilishi kwenye Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC), Sitta alisema katika vikao vyote vya majadiliano visiwa hivyo vimekuwa na uwakilishi.

Isitoshe akasema kuwa katika kuthamini Zanzbar, EAC inajiandaa kuwekza katika miradi mitatu visiwani humo ambayo ni ujenzi wa kiwanja cha ndege cha kimataifa Pemba, ujenzi wa Bandari ya Maruhubi na chelezo ya kusafirisha mizigo na magari Zanzibar, Mombasa na Dar es Salaam.

SOURCE:MWANANCHI

Serikali imechukua hatua kuhusu ripoti za CAG?

Elias Msuya
KWA muda mrefu sasa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa fedha za serikali (CAG) amekuwa akieleza jinsi idara mbalimbali za serikali zinavyotumia vibaya fedha za walipa kodi.Lakini taarifa hizo, serikali inaziona kama porojo tu. Kwanini? Kwa sababu hakuna hatua zozote zinazochukuliwa na serikali dhidi ya watendaji wake wanaohusika.

Kwa mfano taarifa iliyotolewa na CAG kwa wajumbe wa mkutano cha chama cha Serikali za Mitaa – ALAT, walipokutana Dar es Salaam hivi karibuni inaonesha kuwepo kwa ubadhirifu mkubwa wa fedha na rasilimali katika halmashauri nyingi nchini.Alitaja halmashauri tano zinazoonekana vinara kuwa ni pamoja na Rombo, Kilosa, Rorya, Tarime na Manispaa ya Sumbawanga.

Alitoa mfano wa posho za safari walizolipana watendaji kwa halmashauri za Rombo na Kilosa, akisema kulikuwa na Sh 203,379,000 zilizolipwa isivyo halali huku madaftari ya mahudhurio yakionesha kuwa watumishi hao walikuwepo kazini kwenye vituo vyao.

Katika Halmashauri ya Wilaya ya Rombo mafuta ya magari yenye thamani ya Sh 64,581,030 yanaonekana kutumika bila kuwa na maelezo sahihi.Kwa upande wa elimu taarifa hiyo inaonesha kuwa watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo walitumia vibaya fedha za elimu kiasi cha Sh 31,020,000, ikijumuisha tuhuma za wizi wa wino wa mashine ya chapa wenye thamani ya Sh.14,635,000 na wino wa mashine ya kutolea nakala wenye thamani ya Sh 16,385,000.

Vilevile imeonyesha kukosekana kwa hati za malipo zenye thamani ya sh 766,489,920 wakati wa ukaguzi katika Halmashauri ya wilaya ya Kilosa.Kama hiyo haitoshi CAG ametaja matukio sita ya wizi wa fedha katika halmashauri ya Wilaya ya Kilosa yanayohusiana na ubadhirifu wa fedha wa kiasi cha Sh 277,026,849 uliosababishwa na udhaifu katika udhibiti wa mfumo wa ndani wa halmashauri ambapo, usuluhisho wa benki ulifanywa na watumishi wasio waaminifu, pia haukutengenezwa kwa wakati.

Kulikuwa pia na malipo ya awali kwa wakandarasi kinyume na kiwango kinachokubalika ambapo baadhi ya wakandarasi wilayani Kilosa walikuwa wakipewa malipo ya awali kwa kiwango cha asilimia 30 hadi 70 ya fedha ya mkataba kinyume na kiwango cha asilimia 15 kilichoidhinishwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma( PPRA).

Wilaya hiyo pia imepata hasara katika ukusanyaji wa mapato ambapo imetumia jumla ya Sh 119,614,000 ili kukusanya kiasi cha Sh.57,226,690 hivyo kusababisha hasara ya Sh.62,387,110.Mbali na kupata hasara kwenye wilaya hizo kumekuwa pia na tatizo la kutoingiza mapato kwenye vitabu vya fedha. Kwa mfano kiasi cha Sh 7,380,000 kilichopatikana kutokana na mauzo ya viwanja katika mji wa Holili uliopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Rombo hazikuingizwa katika vitabu vya fedha vya Halmashauri.

Kiasi hiki kinajumuisha Sh2,785,000 ambazo zilitokana na wizi wa kutumia kalamu na Sh4,595,000 zilizowekwa kwenye akaunti ya mtu binafsi.Hizo ni baadhi tu ya takwimu zilizotajwa na CAG hasa kwa kuwa ndiyo zimeshikilia rekodi ya ubadhirifu. Lakini upo ubadhirifu mwingine mwingi tu unaoendelea katika halmahsauri za wilaya na manispaa nchini.

Licha ya kuwepo kwa ofisi ya mkaguzi na mdhibiti wa fedha za serikali anayejitahidi kufichua uozo huo, serikali imekaa kimya.Wakati fedha hizo zikifujwa, hali ya maisha ya wananchi huko vijijini ambao ndiwo walipa kodi hizo zinazofujwa inakatisha tamaa. Wanafunzi hawana madarasa, madawati wala vifaa vya kufundishia. Walimu wanadai malimbikizo ya fedha zao.

Huduma ya maji ni kitendawili kisicho na mteguaji, umeme ndiyo haupo kabisa, barabara hazitamaniki wakati wa mvua. Siyo kwamba fedha hazipo, hapana. Tatizo kuna mchwa kwenye halmashauri hizo ambao kazi yao ni moja tu, kutafuna fedha za umma.

Baadhi ya wakurugenzi kwenye mkutano huo walilalamika kuhamishiwa watendaji walioshindikana kwa wizi na ubadhirifu. Wakibainika kuwa na makosa wanakwenda wizarani na kuomba uhamisho, wanahamia halmashauri nyingine na kuendelea kutafuna kama kawaida. Hayo nayo Waziri wa Tamisemi hayajui?

Siyo kwamba watendaji hao hawajulikani. Hata wakati CAG akitoa taarifa yake waliohusika walikuwa wakimsikiliza na mwisho wa yote wamekomba marupurupu ya semina na kuondoka.

Mawaziri nao walikuwepo kwenye mkutano huo. Waziri mkuu Mizengo Pinda ndiye aliyefungua mkutano huo. Walikuwepo pia Waziri wa Sheria na Katiba Celina Kombani, Naibu Waziri wa Tamisemi Aggrey Mwanri na Waziri wa nchi katika ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu Steven Wassira.Wamesikiliza uozo huo na wamekuwa wakiusikia mara kwa mara, lakini hakuna hatua yoyote inayochukuliwa.

Nilitegemea kusikia katika mkutano huo, walau wajumbe wakatoka na azimio la kuwawajibisha wafujaji wa fedha za umma ili kujenga upya msingi wa maendeleo, lakini hakuna lolote.

Hii inaonyesha kuwa serikali yetu imejaa viongozi wa maneno, wasiojua kuchukua hatua hata kwenye makosa ya wazi.Nadhani hii sasa inatosha. Kama viongozi waliingia madarakani kuwatumikia Watanzania hebu wachukue hatua ili kunusuru maisha ya Watanzania yaliyozama kwenye ufisadi.

Elias Msuya ni mwandishi wa makala wa gazeti la mnwananchi; 0754 897 287

Uhuru:Tujenge timu, hakuna aliyehongwa

Sosthenes Nyoni
WINGA wa kimataifa wa Tanzania na klabu ya Simba, Uhuru Selemani amewasihi mashabiki na viongozi wa timu hiyo kuacha tabia ya kuwahukumu wachezaji kwamba walihujumu na kufungwa na wapinzani wao Yanga bao 1-0 kwenye fainali ya Kombe la Kagame iliyofanyika Jumapili iliyopita kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Kauli ya nyota huyo ambaye hivi karibuni amerejea dimbani baada ya kupona goti lililokuwa linamsumbua inafuatia kitendo cha baadhi ya mashabiki wa Simba kuwatuhumu baadhi ya wachezaji kuwa ndio sababu ya timu yao kufungwa na Yanga siku ya fainali.

Wachezaji wa Simba wanaoshutumiwa na mashabiki kuwa walifanya hujuma na kuchangia timu hiyo kufanya vibaya ni kiungo Mohamed Banka, mshambuliaji Musa Hassan Mgosi na beki Kelvin Yondani.

Simba ilikuwa haipewi hata nafasi ya kufika kwenye raundi ya pili kutokana na kuwa na kikosi dhaifu baada ya kutimua nyota wake wengi siku chake kabla ya michuano hiyo, lakini wachezaji hao waliweza kupigana na kufika fainali.

Akizungumza na Mwananchi jijini Dar es Salaam jana Uhuru alisema kitendo cha kuwahukumu wachezaji katika mchezo mmoja tu kinaonyesha jinsi gani mashabiki wa timu hiyo hawana uvumilivu na kusahau mazuri yaliyofanywa na wanaowatuhumu katika siku za nyuma.

"Mpira hauko hivyo mashabiki wanatakiwa waelewe hauwezi kucheza vizuri siku zote, kuwalaumu wachezaji fulani sio sahihi na hii inaonyesha ni jinsi gani tunavyokosa uvumilivu na kusahau mazuri yaliyofanywa na hawa hawa tunaowalaumu."

"Kwa mfano Mgosi mimi namjua vizuri sana na yeye ananifahamu, nina uhakika tukianza kucheza pamoja atafunga mabao mengi, wewe subiri ligi ianze," alisema Uhuru.

Selemani pia aliwaasa viongozi kuacha fikra za kuwafukuza wachezaji kutokana na matokeo yao na Yanga na badala yake waimarishe kikosi ili kiweze kufanya vizuri msimu ujao.

"Sawa inawezekana labda kuna ambao viwango vyao vimeshuka, lakini hili la kumwacha mchezaji kwa sababu ya matokeo ya mechi ya Simba na Yanga sio sahihi, hapa watatakiwa kutafakari kwa makini na pia ni vizuri kuimarisha timu ili iweze kufanya vizuri msimu ujao,"alisema Uhuru.

Akizungumzia sakata la kutaka kuachwa na Simba kiungo Banka, alilimbia gazeti hili kwa simu yake ya mkononi , "mimi sina taarifa rasmi zinazohusiana na kutemwa na klabu hiyo zaidi ya kusoma na kusikia kupitia vyombo vya habari kama watu wengine."

"Sina cha kuongea ndugu yangu kuhusu hilo kwa sababu sina taarifa rasmi za kiofisi, hebu ngoja tusubiri tuone kitakachotokea,"alimaliza Banka ambaye alicheza mechi zote za Simba kwenye kikosi cha kwanza kwenye mashindano ya Kagame, Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho msimu huu.

Imekuwa ni jambo la kawaida kwa viongozi wa Simba na Yanga kuwashutumu wachezaji wao kwamba wamehongwa au kuhujumu mechi kila timu hizo zinapocheza na moja kufungwa, hakuna upande huwa unakubali matokeo hayo yalikuwa ya uwanjani.

Sita wafa maji, wawili walipuliwa kwa bomu

Joyce Joliga, Songea
WATU wanane wamekufa katika matukio mawili tofauti yaliyotokea mkoani Ruvuma, wakiwamo sita waliokufa maji katika Ziwa Nyasa na wawili waliolipukiwa na bomu.Habari zilizolifikia gazeti hili jana zilieleza kuwa wakati watu hao sita walifariki , wengine sita walinusurika kifo baada ya boti waliyokuwa wakisafiria kuzama katika Ziwa Nyasa wilayani Mbinga, kutokana na ziwa hilo kuchafuka kutokana na upepo mkali.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Michael Kamuhanda alisema jana kuwa boti hiyo iliondoka katika bandari ndogo ya Mbamba Bay tangu Julai 11 ikiwa na abiria 12, ikielekea Malawi.

Akifafanua zaidi Kamanda Kamuhanda alisema, ikiwa katikati ya ziwa ilizama na kusababisha watu sita kufa papo hapo na wengine sita kuokolewa baada ya kuogelea kwa umbali mrefu kwa kutumia madumu ya mafuta waliyokuwa nayo katika boti hiyo.Kwa mujibu wa Kamanda Kamuhanda, waliokufa ni Mussa Moses, Daniel Wilson, Kimanda Charahani, Vincent Kambona, Kassim Matembo pamoja na mwingine mmoja ambaye jina lake hadi sasa halijatambulika.

Aliwataja waliookolewa kuwa ni pamoja na Titus Mwakasegye (32), Anna Kalima (35), John Kamanga (36), John Komba (36), Davis Mapunda (33) na Michael Rombola (37), ambao wote wamelazwa katika Kituo cha Afya cha Mbamba Bay na hali zao zinaendelea vizuri.

Katika tukio hilo, kamanda alisema boti hiyo, mali ya Frank Sumuni, raia wa Tanzania, ilikumbwa na madhara hayo ambapo baada ya muda mrefu kupita bila mawasiliano, wafanyakazi wa bandari walitoa taarifa polisi na ndipo juhudi za kuanza kuwatafuta zilianza na kufanikiwakuwaokoa watu hao sita.

Baada ya uokoaji huo, Kamanda Kamuhanda alisema watu hao walikimbizwa katika kituo cha afya cha Mbamba Bay kupatiwa matibabu na kuongeza kwamba, Jeshi la Polisi mkoani humo linaendelea kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini chanzo cha ajali hiyo.

Kufuatia tukio hilo, kamnada huyo aliwashauri wamiliki wa vyombo vya usafiri majini kuacha kubeba mzigo mkubwa kuliko uwezo wao ikiwa ni pamoja na kuweka vifaa vya uokoaji katika boti zao ili pindi kunapotokea matatizo watu wapate vyombo vya kujiokolea.

Hii ni mara ya pili kwa wiki hii kutokea kwa ajali katika Ziwa Nyasa ambapo juzi raia watatu wa Somalia walikufa maji katika ziwa hilo na kufanya idadi ya watu waliokufa maji kwa wiki hii kufikia tisa na wengine 84 kunusurika kutokana na vyombo vyao vya usafiri kuzama wakiwa safarini kwenda Malawi.

Katika hatua nyingine, wakazi wa Wilaya ya Songea Vijijini mkoani Ruvuma wamepatwa na hofu baada ya wananchi wawili kufariki dunia baada ya kulipuliwa na bomu na vichwa vyao kupasuliwa vipande vipande na viungo vyao kutupwa ovyo baada ya bomu waliloliokota kichakani kwa lengo la kuchomea matofali kulipuka ghafla na kusababisha vifo.

Tukio hilo lilitokea jana katika Kijiji cha Mpitimbi B ambako watu hao ambao wanadaiwa ni mafundi wa kufyatua matofali walipokuwa wakiendelea na shuguli zao katika moja ya vichaka vya kijiji hicho.

Akizungumza na Mwananchi jana, Kamanda Kamuhanda aliwataja watu waliokufa kuwa ni Alfred Luambano (23), mkazi wa kijiji hicho pamoja na rafiki yake ambaye anajulikana kwa jina la Bonge au Chinga (25), mkazi wa Tunduru ambaye alifika kijijini hapo kwa lengo la kufanya kibarua cha ufyatuaji na uchomaji wa matofali.

Kamanda huyo alisema, "Siku ya tukio Luambano (marehemu), alikwenda kichakani kujisaidia ambapo aliokota kitu kinachodhaniwa kuwa bomu na wakawa wakichezea yeye na mwenzake na ndipo ghafla kilipolipuka.
Akifafanua, alisema bomu hilo lilipasuka na kumlipua kichwani , kusambaratisha miguu na mikono ambako vipande vingine viliruka na kumpasua kichwa huku Bonge naye akifariki papo hapo.

Kwa mujibu wa kamanda huyo, baada ya wananchi kusikia mlipuko huo walianza kukimbia na baadaye walifanikiwa kukuta miili ya marehemu hao ikiwa imeharibiwa vibaya na kitu hicho ambacho kinasadikiwa kuachwa na wapiganaji wa waasi wa Msumbiji wa Renamo wakati wa vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini mwao.Aliwatahadharisha watu kuacha kuchezea vitu wasivyovifahamu na badala yake watoe taarifa kwa vyombo husika, ikiwamo polisi pindi wakatakapobaini uwapo wake.

Wakati huo huo, baadhi ya wananchi wametoa maoni yao ambapo wameiomba Serikali kutuma timu ya wataalam wa mabomu toka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) au Polisi kufanya uchunguzi katika eneo hilo ili kuweza kuchunguza kama bado kuna mabaki ya mabomu ili yaweze kuangamizwa ili kupunguza hofu kwa wananchi ambao maeneo wanayoishi yalikuwa yakihifadhiwa mabomu hayo.

Kwa upande wake, Wilbert Mahundi alisema amesikitishwa na tukio hilo na aliiomba Serikali isaidie kupeleka mbwa wa kunusa mabomu katika maeneo ya Mpitimbi na Muhukuru ili wasaidie kuyatafuta ili yasiendelee kuwaathiri wananchi na kuwasababishia kuishi kwa woga.

Tanesco waingiza mitambo ya kufulia umeme

Elizabeth Ernest
SHIRIKA la Umeme Tanzania (Tanesco), limeanza kuingiza mitambo yenye thamani ya Dola 120 milioni za Marekani kwa ajili ya kufulia umeme, katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Meneja Mahusiano kwa Umma katika Tanesco, Badra Masoud, mitambo hiyo itatumia gesi asilia kuzalishia umeme kwa kiwango cha megawati 100.

Alisema kwa sasa shirika lina upungufu wa megawati 250 za umeme yakiwa ni matokeo ya kupungua kwa kina cha maji katika Mabwawa ya Kidatu na Mtera.

Badra ambaye alikuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, alisema tayari shirika limeshaingiza mtambo mmoja na mingine miwili itaingia wakati wowote kuanzia sasa.

Pia alisema kiwango cha mgawo wa umeme kimeongezeka kwa saa 18 badala ya 12 na kwamba hiyo inatokana na sababu za kitaalamu, zilizolilazimisha shirika kuzima mitambo ya uzalishaji.

"Wananchi wamekosa imani na Tanesco hata wanapotuona hii ni kutokana na mgawo wa umeme unaoendelea lakini tuna jitihada tunazozifanya ili kutatua tatizo hili hatujakaa kimya,"alisema.


Pia alisema, Tanesco inalazimika kukupunguza mgawo katika baadhi ya maeneo kutokana na ukame katika mabwawa.

Alisema mitambo hiyo iliyoingia ina uwezo wa kuzalisha megawati 34 na kwamba itakapofungwa pamoja na ile itakayooingizwa baadaye, itazalisha megawati 100.

Alisema inatarajiwa kuwa kazi ya kufunga mitambo hiyo, itakamilika Desemba mwaka huu.

Badra alisema mitambo hiyo itakayofungwa na Kampuni ya Jacob Sen Elektro, itasaidia kuongeza kiwango cha umeme katika gridi ya taifa na kupunguza tatizo la nishati.

Alisema, pamoja na mitambo hiyo, Tanesco pia itakodisha mitambo ya Agreco itakayoingizwa nchini Agosti mwaka huu kwa ajili ya kuzalisha megawati 100 za umme.

"Serikali inashughulikia mafuta kwa ajili ya kuzalisha mitambo ya IPTL ambayo pia itazalisha umeme wa megawati 100 kwa hiyo tatizo lililopo litakuwa limepungua kwa kiasi kikubwa au kumalizika kabisa,"alisema.

Meneja mkandarasi wa Jacob Sen Elektro, French Richard, alisema tayari wamekwishaanza kujenga maeneo ya kufunga mitambo hiyo na kwamba mitambo iliyosalia inategemewa kuletwa nchini Jumamosi.

Friday, July 8, 2011

Sumaye: Mafisadi lazima watoswe


ASEMA CCM NI CHAMA CHA WANYONGE
Daniel Mjema, Moshi
WAZIRI Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, amesema tofauti ya kipato kati ya matajiri na masikini, rushwa na ufisadi vinatishia mustakabali wa amani nchini na kusisitiza kuwa mafisadi ndani ya CCM lazima watoswe.Sumaye alitoa kauli hiyo jana katika viwanja vya Soko la Pasua, mjini Moshi alipokuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya chama cha TANU kutimiza miaka 57 tangu kuanzishwa kwake.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali CCM na Serikali, akiwamo Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Meja Jenerali Mstaafu Said Kalembo, Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Alhaji Mussa Samizi na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Vicky Swai.

“CCM ni chama cha wanyonge kwa maana yawafanyakazi, wakulima na wafanyabiashara wanaofanya biashara halali…. Lakini kuna dalili inayoonyesha kuwa CCM sasa kimeanza kutekwa na wachache wenye uwezo wa kifedha,” alisema Sumaye.

Katika hotuba hiyo iliyovuta hisia za wananchi na wanachama wa CCM waliohudhuria mkutano huo, Sumaye alisema japokuwa mambo hayo yanauma, lakini ni lazima WanaCCM waelezane kuhusu mwelekeo wa chama chao.

“Mwelekeo huu ni hatari kwa chama chetu na kwa mustakabali wa taifa letu…,tusijidanganye ni lazima tujue kuwa Watanzania wengi wanaitegemea CCM, hivyo lazima ikae katika msingi unaoeleweka… Hatuwapigi vita wala kuwachukia matajiri ila ila wasikiteke nyara chama,”alisisitiza Sumaye.

Jambo lingine alilosema ni hatari kwa mustakabali wa nchi, ni mgawanyo mbaya wa utajiri akisema katika nchi yoyote duniani, lazima watakuwepo matajiri na masikini, lakini tatizo ni pale kundi dogo linapohodhi utajiri wa nchi husika.

“Tatizo hapa ni kundi la watu wachache wanapotaka kuhodhi utajiri wa nchi… Hali hiyo si salama kwa matajiri na si salama kwa masikini na wala si salama kwa nchi nzima,” alisema sumaye huku akishangiliwa na wana CCM na wananchi wengine.

Aliongeza kusema”wale wasionacho kama ikitokea na dalili hiyo imeanza kujitokeza katika nchi yetu …wale masikini watapigana na wale walionacho bila kujali kama ulichonacho ulikipata kwa halali ama la”.

Sumaye aliwataka Watanzania kutofikia huko na kudokeza TANU ililisimamia vizuri jambo hilo na CCM ni lazima nayo ilisimamie akisema taifa ni lazima lijenge mfumo utaohakikisha utajiri hauwi kwa watu wachache kwani hiyo ni hatari kwa amani.

Kuhusu suala la rushwa ambalo limekuwa likipigiwa keleke nchi nzima, Sumaye alisema tatizo hilo limeanza kuota mizizi nchini na kwamba, kama Watanzania hawatakuwa na ujasiri wa kuikata basi utaiua CCM na nchi.

“Tutaua chama chetu na hata nchi yetu….ni lazima tuwe na ujasiri wa kukata mizizi ya rushwa….tusiposimama kidete huduma za jamii zitakuwa zinapatikana katika kundi la watu wachache wenye uwezo wa kifedha,”alisema Sumaye.

Sumaye alisema Ufisadi ni mbaya zaidi kuliko wizi akisema tatizo hilo lipo nchini na linaonekana kukua kwa kasi na kushika mizizi kwa nguvu.

Hata hivyo alimpongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kile alichosema ni ujasiri wake wa kulikemea suala hilo kwa nguvu zote za kutoa maelekezo kwa CCM kujivua gamba akisema “kama Rais wa nchi amefikia mahali akalisemea basi tatizo ni kubwa”.

“Marehemu mzee Rashid Mfaume Kawawa Mungu amrehemu aliwahi kutuambia kama mnasafiri katika mtumbwi mmoja na mnamuona mwenzenu anaanza kuutoboa mtumbwi basi mtoseni yeye baharini vinginevyo wote mtazama,”alisema.

Sumaye alifafanua kuwa Mtumbwi wa CCM ndio umebeba Watanzania wote hivyo ni azima uwe salama na kwamba CCM haitakubali mtu au kundi la watu kuutoboa mtumbwi huo ili watanzania wote wazame na kusisitiza lazima mtu huyo atoswe.

Kauli hiyo ya Sumaye ilionekana kuunga mkono tamko la Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) lililowataka wanachama wa chama hicho wanaotuhumiwa kwa ufisadi wakiwemo Wabunge, kujiuzulu wenyewe vinginevyo CCM itawawajibisha.

Lakini mbali na tamko hilo, lakini kauli ya Sumaye ambaye anaonekana kuwa na nguvu ndani ya CCM imekuja wakati kuna sakata la ufisadi katika ununuzi wa rada ambapo Mwanasheria mkuu wa serikali wa zamani, Andrew Chenge anatajwa.

Vyombo vya habari jana vilimkariri katibu Mkuu wa chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), Dk. Wilbroad Slaa na Waziri kivuli wa sheria na mambo ya katiba, Tundu Lissu wakisisitiza upo ushahidi wa kumtia hatiani Chenge.

Chenge mwenyewe mara zote amekanusha tuhuma hizo na jana alikaririwa akiwataka wenye ushahidi kuuwasilisha Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa(TAKUKURU) huku akisema uchunguzi wa tuhuma hizo ulishafungwa.

Simba yanusa ubingwa


Sosthenes Nyoni na Sweetbert Lukonge
MABINGWA mara sita,
Simba wamefanikiwa kulipiza kisasi cha mwaka 1994 baada ya kuichapa El Merreikh kwa mikwaju ya penalti 5-4 na kutinga hatua ya fainali ya Kagame Castle Cup na sasa inamsubili mshindi wa leo kati ya Yanga na St George.

Katika mchezo huo ulishudia timu hizo zikienda dakika 120 baada ya kutoka ya bao 1-1 kwa magoli yaliyofungwa na Adiko Rime dakika 12 kwa El Merreikh kabla ya Ulimboka Mwakingwe kuisawazishia Simba kwa dakika ya 20 kwa kichwa.

Baada ya kutoshana nguvu kwa dakika hizo ndipo changamoto ya mikwaju ya penalti ilitumika kumpata mshindi wa nusu fainali hiyo ya kwanza, lakini kipa wa Simba Juma Kaseja kama kawaida alifanikiwa kudaka penalti ya mwisho na kuwavusha mabingwa hao wa kishitoria kwenye fainali hapo Jumapili.

Wapigaji wa penalti wa Simba waliopata walikuwa Jerry Santo, Salum Kanoni, Ramadhani Nassor 'Chollo', Patrick Mafisango na Ulimboka aliyekosa ni Salum Machaku.

Mabingwa mara mbili El Merreikh wenye walipata wanne ambao ni Faisal Sido, Ahmed Elbasha, Badri Eldin na Essam Elhadary na waliokosa ni Collins Kelechi na Jonas Sakwaha.

Mchezo huo ulianza kwa kasi kwa El Merreikh kufanya mashambulizi ya nguvu baada ya dakika 4, Gala Gabir kupiga shuti la mbali lakini Kaseja alikuwa makini na kupangua mpira huo kabla Partick Mafisango kuondosha hatari hiyo.

Dakika ya 9, Ahmed Elbasha alipiga shuti la umbali wa mita 35, lakini Kaseja alipangua na kuwa kona ambayo haikuwa na madhara kwa Simba.

Mashambuliazi hayo yalizaa matunda kwa El Merreikh baada ya dakika 12, kupata bao la kuongoza kupitia Adiko Rime aliyeunganisha vizuri krosi kutoka upande wa kulia ya Jonas Sekwaha ambayo mabeki wa Simba walikosa umakini kwenye ulinzi.

Kipa wa zamani wa timu ya taifa ya Misri, Isam Elhadary aliendeleza historia yake ya kutoa zawadi ya mabao kwa timu za Tanzania pale alipopangua kizembe krosi ya Shija Mkina na kutua kichwani kwa Ulimboka Mwakingwe aliyeusukimia mpira kimyani kwa kichwa cha kuogelea dakika ya 24.

Kaseja alijikuta akipewa kadi ya njano na mwamuzi Kirwa Syvester kutoka Kenya baada ya kitendo chake cha kupiga mpira nje na kukaa chini kwa madai ya kuumia dakika 45 ili kupoteza muda.

Mkina alishindwa kumalizia vizuri krosi ya Mafisango dakika 52, kabla ya Musa Hassan Mgosi kukosa bao dakika 71, alipojipiga kibuyu na kudondoka mwenye kabla ya mabeki wa El Merreikh kuokoa hatari hiyo jambo lililofanya maelfu ya mashabiki wa Simba uwanjani kushika vichwa wasiamini kilichotokea.

Leo mabingwa mara tatu wa klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati Yanga leo wanashuka uwanjani kupambana na St George ya Ethiopia kutafuta tiketi ya kutinga hatua ya fainali katika mashindano ya kombe la Kagame kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Yanga ambayo mara ya mwisho ilitwaa taji hilo miaka 11 iliyopita mwaka 1999 ilipoifunga SC Villa kwa mikwaju ya penalti itakuwa na kazi ngumu mbele ya St George inayojitambia safu yake ya ushambuliaji katika mashindano ya Kagame.

Kocha wa Yanga, Sam Timbe alisema vijana wake wapo tayari kwa mchezo huo licha ya juzi, kuonyesha kiwango cha chini katika mchezo wa robo fainali dhidi ya Red Sea ya Eritrea.

Hata hivyo Yanga katika mchezo huo ilifanikiwa kuitupa nje ya michuano hiyo Red Sea kwa mikwaju ya penalti baada ya kumaliza dakika 90 kwa suluhu.

Akizungumza na Mwananchi jana Timbe ambaye ni kocha pekee mwenye rekodi ya kulitwaa kombe hilo mara tatu akiwa na timu tofauti tofauti alisema tayari ameshayafanyia kazi mapungufu yote yaliyojitokeza katika mchezo dhidi ya Red Sea.

"Mchezo wa kesho (leo) utakuwa ni mgumu, lakini vijana wangu tayari wapo vizuri kupambana na kuhakikisha tunaibuka na ushindi katika mechi hiyo ambayo ni muhimu kwetu kushinda ili tuweze kutinga fainali.

"Tayari nimeshayafanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza katika mchezo wetu dhidi ya Red Sea ni matumaini yetu kuwa tutashinda mchezo huo licha ya wapinzani wetu kihistoria kuonekana ni timu nzuri zaidi katika ukanda wetu wa Afrika Mashariki na Kati," alisema Timbe ambaye pia aliwahi kuchukua ubingwa wa michuano hii akiwa mchezaji wa timu ya KCC ya Uganda.

Alisema kiufundi vijana wake wote wapo vizuri hakuna majeruhi na anatarajia kutumia mifumo yake ya kila siku ambapo ataanza na 4-4-2 na akiona mambo yanakuwa tofauti atalazimika kubadili na kutumia 4-3-3 ili kuhakikisha anaibuka na ushindi.

Hivi Wassira amekuwa mufilisi wa hoja?


KATIKA toleo la jana la gazeti hili, tulichapisha habari zilizomnukuu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia masuala ya mahusiano na uratibu, Stephen Wassira akilishambulia vikali gazeti hili kwa kuchapisha picha yake gazetini wiki mbili zilizopita akiwa amechapa usingizi bungeni. Alilituhumu kwa kile alichokiita kuandika habari za uchochezi na kwamba lina asili ya nje, hivyo pengine lingependa nchi ikumbwe na vurugu kama ilivyo katika baadhi ya nchi.

Waziri Wassira ambaye alikuwa akifanya majumuisho ya matumizi ya Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu aliongeza: …”tunamwambia umechelewa, hapa hayawezekani”. Wakati anapigwa picha hiyo akiwa anauchapa usingizi, waziri huyo alikuwa anakaimu nafasi ya Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni.

Pamoja na kukiri kuwa alikuwa ameuchapa usingizi wakati Bunge lilikuwa linaendelea, alikiita kitendo cha gazeti hili kuchapisha picha iliyomuonyesha akiwa usingizini kwamba kilikuwa cha uchochezi. Alisema siku hiyo alikuja bungeni akiwa mgonjwa na dawa aliyopewa katika Zahanati ya Bunge ndiyo iliyomuweka katika hali hiyo ya kusinzia.

Lakini waziri huyo alikwenda mbali zaidi na kunukuu vichwa vya habari ambazo gazeti hili lilikuwa limechapisha huko nyuma, akisema zilikuwa za uchochezi. Moja ya habari hizo ilihusu sakata la posho za vikao kwa watumishi wa umma iliyosema kwamba Chadema ilikuwa imeibwaga Serikali. Habari nyingine ni ile iliyomnukuu Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa akisema bungeni kwamba Serikali iliyo madarakani ilikuwa inaogopa kufanya maamuzi.

Tumeorodhesha mlolongo wa tuhuma zilizotolewa na waziri huyo dhidi ya gazeti hili siyo kwa kutaka kuonewa huruma, bali kuwapa fursa wasomaji wetu na wananchi kwa jumla ya kuamua kama kweli gazeti hili linastahili lawama na laana zinazoelekezwa kwake na Waziri Wassira. Rekodi yetu katika muongo mmoja wa kuwapo gazeti hili imeonyesha kuwa, tumekuwa tayari kukosolewa na mara zote tumeomba radhi pale tunapofanya makosa.

Lakini tunapata wasiwasi pale waziri wa serikali anapoweza kupata ujasiri wa kutoa shutuma na tuhuma za uongo dhidi ya gazeti ambalo hata viongozi wa juu wa chama chake cha CCM wanakiri kwamba linaandika ukweli. Kwamba sisi ni wachochezi na gazeti hili lina asili ya nje, hivyo pengine lingependa nchi itumbukie katika vurugu kama ilivyo katika baadhi ya nchi ni tuhuma nzito zinazoweza tu kutolewa na mtu asiyewatakia wenzake mema.

Pamoja na kwamba dhima kubwa ya gazeti hili ni kuwafahamisha na kuwahamasisha wananchi, ukweli ni kwamba gazeti pia linafanya biashara na lishindana kibiashara katika soko ili lipate faida. Ili tuweze kufanikiwa kufanya biashara tunahitaji mazingira mazuri yenye amani, mshikamano na utulivu. Tuhuma za Waziri Wassira kwamba gazeti linataka nchi ikumbwe na vurugu hakika ni kichekesho cha karne.

Pengine tuchukue fursa hii kuwafahamisha wananchi kwamba, tuhuma hizi za waziri huyo ni mwendelezo wa mchezo mchafu wa baadhi ya washindani wetu katika sekta ya umma wenye kusimamia dhana yenye matege kwamba, kwa kuwa wamiliki wa gazeti hili ni wawekezaji kutoka nje, basi waandishi wake hawana uzalendo kwa sababu ajenda wanazotekeleza zinaamuliwa na watu wa nje.

Lakini lazima tuseme tukiwa tunatembea vifua mbele kwamba, waandishi wa habari na wahariri wa Mwananchi na gazeti dada la The Citizen, wanaongozwa na Sera ya Uhariri inayozingatia weledi na inayowapa uhuru kamili wa kuendesha magazeti hayo pasipo kuingiliwa na mtu yeyote. Wasomaji wetu pengine watashangaa kujua kwamba, kati ya wafanyakazi 132 wanaofanya kazi katika magazeti hayo, ni wafanyakazi watatu tu tena wasio na nafasi za kufanya maamuzi ya uhariri ndio wanatoka nje ya nchi.

Tungependa kuwahakikishia wasomaji wetu na wananchi kwa jumla kwamba, hatutarudi nyuma katika kusimamia ukweli na tutafanya hivyo bila woga wala upendeleo. Kwa upande wa wabunge wanaochapa usingizi bungeni, tunawapa tahadhari kuwa tutawachongea kwa wapigakura wao ili siku ikifika wafanye maamuzi magumu.

'Serikali haitaingia gharama kutafiti mafuta,gesi'


Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, amesema Serikali ya Tanzania haitaingia gharama zozote wakati meli ya Poisedon, itakapokuwa inafanya uchunguzi wa mafuta na gesi katika pwani ya Tanzania.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Pinda alitoa kauli hiyo jana baada ya kutembelea eneo la viwanda vya kujenga meli ili kuona hatua mbalimbali za ujenzi wa meli na kuikagua meli ya uchimbaji mafuta.

Meli hiyo ya Poisedon inajengwa katika Bandari ya Geoje, Kusini Mashariki mwa Seoul, Korea Kusini.

Waziri Mkuu anatarajiwa kuizindua meli hiyo leo saa 4 asubuhi katika Bandari ya Geoje.

Alisema wanachofanya sasa wataalamu kutoka Kampuni ya Petrobas ya Brazil ni kutafiti na kubainisha maeneo mawili ambako meli hiyo itachimba endapo matokeo yatakuwa mazuri.


"Tunaishukuru Serikali ya Brazil kwa kuamua kuisadia Serikali ya Tanzania kufanya utafiti huo muhimu," alisema Waziri Mkuu Pinda.

Alisema hatua hiyo ni dalili njema kuwa uwekezaji unawezekana kufanyika Tanzania na kuahidi kuwa Serikali ya Tanzania itafanya kila iwezalo, kuweka ulinzi wakati wataalamu hao wakiwa kazini ili kuzuia hatari ya kupambana na maharamia.

Mapema, akitoa taarifa kwa Waziri Mkuu kuhusu ujenzi wa meli hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni Petrobas Tanzania, Samuel Miranda, alisema wanatarajia kwamba meli hiyo itafanya kazi katika ukanda wa pwani kwa muda wa miezi 20 katika maeneo ya kati ya Mafia na Mtwara.

Kuhusu uendelezaji wa miundombinu, Miranda alisema hadi sasa wameshawekeza kiasi cha dola za Marekani milioni 11 na ifikapo Desemba mwaka huu watatoa Dola za Marekani milioni 14 ili kuendeleza Bandari ya Mtwara.

Kuhusu utoaji ajira kwa Watanzania, alisema wameanza kutoa mafunzo kwa vijana 50 wa kike na wa kiume wa kutoka Mtwara ambao wakifaulu, watafanya kazi katika meli hiyo.

"Meli hii itakuwa Mtwara na tunatarajia kuanza kazi mwanzoni mwa Septemba. Tumeanza na vijana 50 kuanzia Julai mosi, watapewa mafunzo maalumU ya miezi mitatu ya umeme, umakenika na masuala ya uchimbaji mafuta na si kitu kingine," alifafanua.

"Mafunzo haya yanaendeshwa kwa ubia baina ya TPDC, Veta, Petrobas na Taasisi ya Cenal ya Brazili ambayo inafanana na Veta ya hapa Tanzania, nia yetu ni kupata wakufunzi ambao wataendelea kufundisha vijana wengi zaidi katika fani hii,"alisema.

Mbali na hatua hiyo, Miranda alisema wana mkataba na wahandisi wanne wa Kitanzania ambao tayari wamepelekwa Brazil kwa mafunzo ya muda mfupi na kisha watapelekwa Uingereza ili kujifunza zaidi masuala ya uchimbaji mafuta.

Meneja Mradi wa Kampuni ya Ocean Rig ya Uingereza inayosimamia ujenzi wa meli hiyo, David Gray, alimweleza Waziri Mkuu kwamba kwamba meli hiyo yenye urefu wa mita 242 na upana wa mita 52, imegharimu Dola za Marekani milioni 800.
SOURCE:Mwananchi