Friday, July 8, 2011

Simba yanusa ubingwa


Sosthenes Nyoni na Sweetbert Lukonge
MABINGWA mara sita,
Simba wamefanikiwa kulipiza kisasi cha mwaka 1994 baada ya kuichapa El Merreikh kwa mikwaju ya penalti 5-4 na kutinga hatua ya fainali ya Kagame Castle Cup na sasa inamsubili mshindi wa leo kati ya Yanga na St George.

Katika mchezo huo ulishudia timu hizo zikienda dakika 120 baada ya kutoka ya bao 1-1 kwa magoli yaliyofungwa na Adiko Rime dakika 12 kwa El Merreikh kabla ya Ulimboka Mwakingwe kuisawazishia Simba kwa dakika ya 20 kwa kichwa.

Baada ya kutoshana nguvu kwa dakika hizo ndipo changamoto ya mikwaju ya penalti ilitumika kumpata mshindi wa nusu fainali hiyo ya kwanza, lakini kipa wa Simba Juma Kaseja kama kawaida alifanikiwa kudaka penalti ya mwisho na kuwavusha mabingwa hao wa kishitoria kwenye fainali hapo Jumapili.

Wapigaji wa penalti wa Simba waliopata walikuwa Jerry Santo, Salum Kanoni, Ramadhani Nassor 'Chollo', Patrick Mafisango na Ulimboka aliyekosa ni Salum Machaku.

Mabingwa mara mbili El Merreikh wenye walipata wanne ambao ni Faisal Sido, Ahmed Elbasha, Badri Eldin na Essam Elhadary na waliokosa ni Collins Kelechi na Jonas Sakwaha.

Mchezo huo ulianza kwa kasi kwa El Merreikh kufanya mashambulizi ya nguvu baada ya dakika 4, Gala Gabir kupiga shuti la mbali lakini Kaseja alikuwa makini na kupangua mpira huo kabla Partick Mafisango kuondosha hatari hiyo.

Dakika ya 9, Ahmed Elbasha alipiga shuti la umbali wa mita 35, lakini Kaseja alipangua na kuwa kona ambayo haikuwa na madhara kwa Simba.

Mashambuliazi hayo yalizaa matunda kwa El Merreikh baada ya dakika 12, kupata bao la kuongoza kupitia Adiko Rime aliyeunganisha vizuri krosi kutoka upande wa kulia ya Jonas Sekwaha ambayo mabeki wa Simba walikosa umakini kwenye ulinzi.

Kipa wa zamani wa timu ya taifa ya Misri, Isam Elhadary aliendeleza historia yake ya kutoa zawadi ya mabao kwa timu za Tanzania pale alipopangua kizembe krosi ya Shija Mkina na kutua kichwani kwa Ulimboka Mwakingwe aliyeusukimia mpira kimyani kwa kichwa cha kuogelea dakika ya 24.

Kaseja alijikuta akipewa kadi ya njano na mwamuzi Kirwa Syvester kutoka Kenya baada ya kitendo chake cha kupiga mpira nje na kukaa chini kwa madai ya kuumia dakika 45 ili kupoteza muda.

Mkina alishindwa kumalizia vizuri krosi ya Mafisango dakika 52, kabla ya Musa Hassan Mgosi kukosa bao dakika 71, alipojipiga kibuyu na kudondoka mwenye kabla ya mabeki wa El Merreikh kuokoa hatari hiyo jambo lililofanya maelfu ya mashabiki wa Simba uwanjani kushika vichwa wasiamini kilichotokea.

Leo mabingwa mara tatu wa klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati Yanga leo wanashuka uwanjani kupambana na St George ya Ethiopia kutafuta tiketi ya kutinga hatua ya fainali katika mashindano ya kombe la Kagame kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Yanga ambayo mara ya mwisho ilitwaa taji hilo miaka 11 iliyopita mwaka 1999 ilipoifunga SC Villa kwa mikwaju ya penalti itakuwa na kazi ngumu mbele ya St George inayojitambia safu yake ya ushambuliaji katika mashindano ya Kagame.

Kocha wa Yanga, Sam Timbe alisema vijana wake wapo tayari kwa mchezo huo licha ya juzi, kuonyesha kiwango cha chini katika mchezo wa robo fainali dhidi ya Red Sea ya Eritrea.

Hata hivyo Yanga katika mchezo huo ilifanikiwa kuitupa nje ya michuano hiyo Red Sea kwa mikwaju ya penalti baada ya kumaliza dakika 90 kwa suluhu.

Akizungumza na Mwananchi jana Timbe ambaye ni kocha pekee mwenye rekodi ya kulitwaa kombe hilo mara tatu akiwa na timu tofauti tofauti alisema tayari ameshayafanyia kazi mapungufu yote yaliyojitokeza katika mchezo dhidi ya Red Sea.

"Mchezo wa kesho (leo) utakuwa ni mgumu, lakini vijana wangu tayari wapo vizuri kupambana na kuhakikisha tunaibuka na ushindi katika mechi hiyo ambayo ni muhimu kwetu kushinda ili tuweze kutinga fainali.

"Tayari nimeshayafanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza katika mchezo wetu dhidi ya Red Sea ni matumaini yetu kuwa tutashinda mchezo huo licha ya wapinzani wetu kihistoria kuonekana ni timu nzuri zaidi katika ukanda wetu wa Afrika Mashariki na Kati," alisema Timbe ambaye pia aliwahi kuchukua ubingwa wa michuano hii akiwa mchezaji wa timu ya KCC ya Uganda.

Alisema kiufundi vijana wake wote wapo vizuri hakuna majeruhi na anatarajia kutumia mifumo yake ya kila siku ambapo ataanza na 4-4-2 na akiona mambo yanakuwa tofauti atalazimika kubadili na kutumia 4-3-3 ili kuhakikisha anaibuka na ushindi.

No comments: