Wednesday, November 10, 2010

Shibuda aifunda CCM mtifuano wa spika

na Mwandishi wetu




p>MBUNGE mteule wa Maswa Magharibi, John Shibuda (CHADEMA), amewatahadharisha wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kufanya maamuzi ya busara wakati wa kupitisha jina la mtu atakayewania kiti cha uspika, vinginevyo watakisambaratisha chama hicho.
Shibuda alisema hayo jana wakati akizungumza na gazeti hili, katika viwanja vya Bunge, mjini Dodoma.

Alisema kuna kila sababu ya CCM kuwa makini katika kupitisha jina la Spika, vinginevyo watakuwa wanatengeneza mwanya wa kukisambaratisha chama hicho.

Bila kutaja majina, Shibuda alisema inasikitisha kuona nafasi hiyo inagombewa na baadhi ya watu wachafu ambao hawana misingi ya uongozi na wanaonyesha wazi walivyo na uchu wa kupata nafasi hiyo, huku wakiwa na mawazo ya kulipiza kisasi.

Alimtaka Rais Kikwete kuhakikisha analisimamia jambo hilo kwa makini na kudai kuwa iwapo chama tawala kikishindwa kuteua jina la spika makini ambaye anaweza kuongoza nchi ni wazi kuwa kiti hicho kitachukuliwa na kambi ya upinzani.

Kwa sasa mji wa Dodoma umejaa wabunge wanaoonekana kukaaa makundi makundi huku wakijadili ni nani atateuliwa na chama tawala kwa lengo la kugombea nafasi nyeti ya uspika.

Pamoja na kuwapo kwa kampeni kali kati ya vigogo wawili ambao ni spika aliyemaliza muda wake pamoja na waliojitokeza, akiwamo aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Andrew Chenge, lakini bado Watanzania wengi wakiwamo wabunge wa vyama mbalimbali wanasubiri kuona ni nani moshi utafuka vyema kwake.

No comments: