Monday, June 21, 2010

CHADEMA yamkaba koo Mkuu wa Mkoa

na Christopher Nyenyembe, Mbeya



UONGOZI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), umemjia juu Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, John Mwakipesile, kufuatia kauli yake aliyoitoa dhidi ya vijana wa chama hicho, waliohoji namna wawekezaji wa kigeni kutoka China walivyoingia wilayani Chunya na kuanza kuchimba dhahabu.

Hatua hiyo, ilisababisha vijana hao, kupitia Baraza la Umoja la Chama hicho (BAVICHA) wamtake Mwakipesile ajiuzulu kwa vile ameshindwa kutunza mali za wananchi kama Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa.

Kutokana na hali hiyo, BAVICHA imemtaka Rais Jakaya Kikwete amwondoe madarakani pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Deodatus Kinawiro, kwa vile wameshindwa kulinda rasilimali ya taifa.

Viongozi hao walitakiwa kujiuzulu kutokana na wao kutokuwa na taarifa za wawekezaji wa Kichina waliokuwa wakichimba dhahabu wilayani Chunya bila kuwa na kibali cha mazingira, huku wakisababisha uharibifu mkubwa wa mazingira.

Hata hivyo, Mwakipesile akijibu hoja za tamko hilo, alisema vijana hao hawana uelewa wa kutosha kuhusiana na mambo ya mkoa wake.

Katika taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa chama hicho, John Mnyika, ilisema kauli na vitendo vya Mwakipesile vinadhihirisha kuwa amelewa madaraka kuliko kuwatumikia wananchi.

“Rais Kikwete anapaswa kumkemea mteule wake na chama chake CCM kinapaswa kumkanya kwa kutoa majibu ya matusi badala ya kujibu hoja za msingi, hili ni tatizo la kuwa na ma-RC na Ma- DC waliokataliwa na wapiga kura, lakini wakateuliwa kwa hisani badala ya uwezo,” alisema Mnyika.

No comments: