Tuesday, September 1, 2009

Mafisadi walitumbukiza fedha Chadema - Mtei


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).



Muasisis wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edwin Mtei, amesema mafisadi wamepenyeza fedha chafu katika chama hicho ili kuvuruga mpango wa kujiimarisha na 'kuchukua' dola.

Mtei, alisema hatua hiyo inapaswa kutambuliwa na kudhibitiwa na vijana wa Chadema, vinginevyo itakiathiri chama hicho na kusababisha kishindwe kufikia malengo yake.

Muasisi huyo ambaye pia ni Mwenyekiti Mstaafu wa Chadema, alisema hayo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha) jijini Dar es Salaam jana.

Mtei ambaye hakuwataja mafisadi hao kwa majina, alisema kuna fedha chafu zilizoingizwa na zitakazoingizwa Chadema kupitia kwa wanachama ama vyama vingine vya siasa hususani vya upinzani, ili kufanikisha ushawishi wenye lengo la kukisambaratisha chama hicho.

“Vijana mjihadhari na mbinu za wale wanaoihujumu nchi ili kujinufaisha, wanatumia fedha chafu ili kuwasambaratisha, watawapaka matope viongozi wenu kwa njia mbalimbali,” alisema na kuongeza kuwa: “Watapenyeza fedha hizo hata kupitia vyama vya upinzani bila hata wenyewe kutambua, ni lazima tutambue kuna vyama vya upinzani vilianzishwa na mafisadi hao ili utawala wao udumu.”

Mtei, alisema ni jukumu la vijana wa Chadema kuvijua vyama hivyo na kubuni mbinu za kuvikabili.

Kwa upande mwingine, Mtei alilalamikia kile alichokiita kuwepo baadhi ya vyombo vya habari, vinavyoshindwa kutekeleza wajibu wenye maslahi kwa nchi badala yake vinatumika kulinda na kutetea maslahi ya mafisadi.

Vilevile, Mtei alisisitiza kuwa kwa kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimekuwepo madarakani kwa takribani miaka 48 bila kufanikisha maisha bora kwa kila Mtanzania, hakuna haja ya kuendelea kujadili uwezo wake, na kwamba njia inayofaa ni kukiondoa madarakani.

Mtei aliyewahi kuwa Waziri wa Fedha na Gavana wa Benki Kuu (BoT) wakati wa utawala wa Serikali ya Awamu ya Kwanza iliyokuwa ikiongozwa na Mwalimu Julius Kambarahe Nyerere, alisema Tanzania ingefanikiwa kufikia ustawi wa jamii na kukuza uchumi wake ikiwa rasilimali za umma kama madini zingetumika ipasavyo.

Alitoa mfano kuwa mikataba ya madini ingesainiwa kwa sharti la Serikali kumiliki asilimia 51 katika kila mgodi nchini, umasikini unaozungumzwa na kushuhudia kwa miongo kadhaa sasa ungekuwa historia.

Naye Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbroad Slaa, alisema azma ya kuchukua dola kutoka CCM ni jukumu zito linalohitaji nyenzo mbalimbali ikiwemo rasilimali watu hasa vijana wenye nguvu, ubunifu na uwezo.

Hata hivyo, Dk Slaa, alisema mazingira yaliyopo Chadema yanaufariji umma kutokana na watu wenye taaluma na viwango tofauti vya elimu na vipaji kujitokeza kwa hiari yao kuwania uongozi wa chama hicho.

“Zamani tulikuwa tunawabembeleza watu, wasomi na vijana walikuwa wanajiunga nasi kwa kificho, wasionekane, waliiogopa CCM na usalama wa taifa, lakini leo watu wanashindana, hakuna woga,” alisema. Alidai hivi sasa Chadema ina maadui wengi wanaoongozwa na CCM, kisha akavishambulia vyombo vya habari (si vyote) kwa kuandika kinyume cha ukweli unaohisiana na chama hicho.

“ Tumendikwa kwamba chama chetu ni cha kidikteta, hata hivyo sikutegemea gazeti ambalo Septemba 15 mwaka 2007 nilimtaja mmiliki wake kuwa ni fisadi, lingeniandika mimi na Chadema kwa uzuri,” alisema bila kulitaja gazeti hilo ama mmiliki wake.

Dk Slaa ambaye pia ni Mbunge wa Kataru, alipuuza taarifa zinazohusu kuchapishwa kwa kitabu kinachomhusu Makamu Mwenyekiti wa zamani wa chama hicho, Marehemu Chacha Zakayo Wangwe, huku kifo hicho kikihusishwa na Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe.

“Chadema haturudi nyuma hata wakiandika vitabu ili kutekeleza mpango wa kutuvuruga...na vijana mnatakiwa kuilinda na kuitetea, isiishie humu ndani, bali jitokezeni hadi kuwania nafasi za uongozi kwenye serikali za mitaa na Uchaguzi Mkuu mwakani,” alisema.

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Kabwe Zitto, alisema hivi sasa Taifa limeelekeza fikra zake katika chaguzi zinazofanyika ndani ya chama hicho, hivyo kuwataka vijana hao kufanya maamuzi muhimu yatakayokiimarisha (Chadema).

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Zitto, wamejitokeza wakiwa pamoja kwa mara ya kwanza, tangu kuanza kwa mchakato wa kuwania Uenyekiti wa chama hicho.

Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, alitangaza kuwania nafasi hiyo, lakini alijitoa baadaye kufuatia ushauri wa wazee wa chama hicho, walioongozwa Mtei.

Zitto na Mbowe aliyebaki kuwa mgombea pekee katika nafasi hiyo, walikutanishwa hadharani jana mbele ya waandishi wa habari na Dk Wilbroad Slaa na Mtei.

Mbowe aliyevaa vazi lake maarufu kama `magwanda ya ukamanda', alikaa kushoto kwa Dk Slaa na Mtei, huku Zitto aliyekuwa amevaa suruali ya jeans na shati za bluu na raba zenye rangi nyeupe na nyeusi kulia kwa viongozi hao.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Slaa alisema kujitoa kwa Zitto kuwania nafasi hiyo, kulitokana na ushauri wa kamati ya wazee wa Chadema, kupitia kanuni zinazotambulika kwenye katiba ya chama hicho.

Slaa, alisema katiba hiyo inatoa haki ya kufikia maamuzi kwa njia ya muafaka, huku kila hatua ya mazungumzo na uamuzi vikiwekwa wazi kwa wanachama wake. Kwa mujibu wa Slaa, uwazi na mwafaka ni miongoni mwa misingi ya demokrasia inayotekelezwa pia na taasisi kama Umoja wa Afrika (AU) na Bunge la Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi zilizo Kusini mwa Afrika (SADC).

“ Sasa kama kuna watu wanadai hatua hiyo imekandamiza demokrasia na ni udikteta, wanatuambia nini kuhusu AU (Umoja wa Afrika) na Bunge la SADC (Jumiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika) ambalo mimi ni mmoja wa wabunge wake? ” Alihoji.

Kwa upande mwingine, alithibitisha kuwapo kwa mgawanyiko uliotokana na Zitto na Mbowe kuwania nafasi hiyo na kusema ni jambo la kawaida katika chaguzi za taasisi yoyote ikiwemo Chadema.

Alisema kufuatia kujitoa kwa Zitto, chama hicho kimezidi kuimarika na kufifisha matumaini ya watu 'waliotabiri' kwamba kitaporomoka.

Naye Mtei, alisema wazee wa Chadema wanatambua uwezo na vipaji vya Zitto na kwamba bado ana mchango mkubwa kwa chama hicho na Taifa.

“ Tunaamini kwamba Zitto ambaye ni mchanga kisiasa bado ana nafasi kwa mwaka 2015 na kuendelea...ataichukua nchi, hivyo tulimuomba aondoe jina akakubali, alionyesha azma yake ya kutaka umoja ndani ya chama,” alisema.

Kwa upande wake, Zitto alisema kujitoa kwake kuwania nafasi hiyo, kulitokana na mazungumzo ya muda mrefu na wazee wa Chadema.

“Lengo letu sote ni kuona chama kinakuwa kimoja, kwa vyovyote vile wazee walioanzisha chama walikuwa na maono yao, nisingependa kukaidi maono yao hivyo nikajitoa bila masharti yoyote,” alisema.

Zitto, alisema kwa kuwa Chadema bado kipo katika mapambano ya kutafuta dola, wanachama wake wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwenye nafasi yoyote na si kugombania vyeo.

Naye Mbowe aliyekuwa anazungumza kwa mara ya kwanza tangu kuanza kwa mzozo huo, alisema ukimya wake ulikusudia kuondoa hatari ya kuwepo kauli ambazo zingechochea mgawanyiko katika chama hicho.

“Mambo mengi yaliandikwa, ikiwemo mimi kutoelewana na kamanda wangu Zitto, kitu ambacho si cha kweli,” alisema.

Hata hivyo, Mbowe aliunga mkono hoja ya Zitto kuhusu nafasi za uongozi kutokuwa lengo la mwanachama kujiunga Chadema.

Alisema nafasi ya uongozi kama Uenyekiti ni jukumu zito lisilokuwa na maslahi yoyote zaidi ya utumishi wa umma katika kufikia malengo waliyojiwekea.

“ Uenyekiti wa Chadema si ulaji, msije mkaandika viongozi watakaochaguliwa watakuwa wameula, hakuna ulaji huku ni kazi kwa kwenda mbele,” alisema.

Mbowe alipinga hoja kadhaa zinazoenezwa dhidi yake, ikiwemo ya kukifanya chama hicho kukosa mtandao hasa mikoani.

Alisema ushiriki wa wanachama katika vikao vya mabaraza ya wazee, wanawake, vijana, Kamati Kuu, Baraza Kuu na Mkutano Mkuu kutoka Tanzania Bara na Visiwani ni uthibitisho wa kuenea kwa Chadema nchi nzima.

No comments: