Wednesday, November 16, 2011

Wabunge: Chadema wanachochea vurugu

SIKU moja baada ya wabunge wa Chadema, kutoka nje ya Bunge na kutoshiriki mjadala wa Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba wa mwaka 2011, wabunge wa CCM na CUF wamepinga hatua hiyo na kusema wenzao hao wana kusudio la kuchochea vurugu na kuvunja Muungano.

Pia wengi wa wabunge hao waliochangia wamemnyooshea kidole Msemaji wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu, kuwa amewapotosha Watanzania na ni mwanasheria na mwanaharakati anayepaswa kurudi shule kusoma na pia ni mchochezi wa kutotaka Muungano na Wazanzibari.

Sambamba na hilo, wabunge hao waliochangia Muswada huo juzi na jana, walitetea madaraka aliyonayo Rais wakisema si makubwa na anastahili kuwa nayo kama kiongozi wa nchi.

Tofauti na wabunge hao wa CCM na CUF, Mbunge wa NCCR-Mageuzi wa Kasulu Mjini, Moses Machali, alikuwa pekee aliyewatetea Chadema kwa uamuzi wao wa kususia majadiliano hayo akisema wametekeleza matakwa ya wananchi.

Miongoni mwa waliochangia mjadala huo ni Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohammed (CUF) aliyesema “ni dhambi isiyosameheka kudharau Wazanzibari waliopiga kura ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa halafu unajifanya wewe (Chadema) ni mkombozi wa watu, Lissu anasema Bunge la kikatiba halitakuwa na haki kwa sababu wabunge wa Zanzibar watashiriki !

“Mna ajenda yenu (Chadema) ya siri, mnaleta ubaguzi ndani ya Bunge, sisi (CUF) ndio tuliandamana kudai Katiba na tulipeleka rasimu ya Katiba, Watanzania wenzangu tusishawishike, maoni ya mabadiliko ya Muswada yametokana na wananchi, taasisi na Kamati ya Bunge, tuaminiane na tupendane,” alisema na kupinga wananchi kuandamana nchi nzima kupinga Muswada huo.

Alihoji kauli ya maoni ya Kambi ya Upinzani kuwa Rais ni dikteta wakati Rais huyo ndiye aliyeleta Katiba hiyo na kufafanua kuwa tangu mwaka 1977 hakuwahi kuona Muswada ulioshirikisha wananchi kama huo.

Alisema madaraka ya Rais yameshapunguzwa vya kutosha kama rasimu ya Katiba kupelekwa kwa wananchi kujadiliwa kabla ya kupitishwa, pamoja na hadidu za rejea kutotungwa na Rais isipokuwa zimeshawekwa kwenye Muswada kitendo ambacho Rais amekikubali.

Kwa upande wa Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Ummy Mwalimu, alilalamikia wanasheria na wanaharakati bungeni kwamba ndio wanapotosha ukweli kwa makusudi na kuwataka kuacha kupinga madaraka ya Rais kwa kumwangalia kama Mwenyekiti wa CCM, bali kama taasisi yenye madaraka na Katiba ya sasa na kuacha kumwita Rais dikteta.

“Mimi nimekuwa mwanaharakati, najua siasa za uanaharakati, waseme huko nyuma kuna maslahi ya nani...wakasome tena wanasheria hawa, si kuleta uchochezi katika nchi yetu,” alisema. Alisema Rais amefanya uungwana kuwaheshimu na kuleta Muswada huo bungeni kwa ajili ya kuunda Tume hiyo, vinginevyo Katiba iliyopo inamruhusu kuunda Tume bila hata kushirikisha wabunge.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM) pamoja na kutaka mamlaka ya Rais yasiingiliwe, alimtaka Lissu anayejiita mwanasheria na mwanaharakati kurudi darasani kuelimika kutokana na kupotosha historia ya nchi kwamba Mwalimu Julius Nyerere alihusika kumomonyoa Muungano kwa kutofuata haki za binadamu, wakati kipengele hicho kiliingizwa kwenye Katiba wakati wa utawala wake na Zanzibar kushirikishwa.

Mbunge wa Gando, Khalifa Suleiman Khalifa (CUF), alisema Chadema wakipata Dola hawatautaka Muungano wala Wazanzibari. Mbunge wa Viti Maalumu, Angela Kairuki (CCM), alishauri wajumbe wa Tume itakayoundwa walipwe kwa mujibu wa kanuni na malipo ya Serikali na si Waziri wa Katiba apange.

Pia Mwenyekiti wa Tume awasilishe ripoti bungeni na si Waziri wa Katiba na misingi na gharama za Bunge la Katiba ziainishwe kwa uwazi kwenye sheria.

Mbunge wa Tabora, Ismail Aden Rage (CCM) alisema wasiokubaliana na Muswada huo wanatafuta mwanya wa kuleta vurugu na kuongeza: “Wanaotaka kuhoji madaraka ya Rais ni wahuni … nimekerwa na kauli ya wenzetu wa Chadema, taarifa ya Lissu inalenga kuvunja Muungano”.

Hata hivyo, Mbunge Machali tofauti na wenzake, aliwatetea akisema “watakaopitisha Muswada huu laana za Watanzania ziwe juu yenu kwa sababu hamkutaka usomwe mara ya pili”.

Alisema wabunge kujikita katika malumbano kunazidi kujenga chuki na aliwatetea Chadema kutoka ukumbi wa Bunge kutokana na kushindwa kuvumilia na walifanya hivyo kupinga mwenendo mzima wa kuwasilishwa Muswada huo.

Katika hatua nyingine, Mbunge wa Mbozi Mashariki, Godfrey Zambi (CCM), aliomba mwongozo wa Spika wa kitendo cha Chadema kutoka nje na kama vyama vingine vitatoka nje, mjadala wa Bunge utaendeleaje. Spika, Anne Makinda alijibu:

“Tumekubaliana mikutano yote ya vyama ifanyike saa 7 mchana na watakaotoka katikati ya mjadala waombe ruhusa, Katibu wa Chadema hajaniomba wakutane baada ya kipindi cha maswali, nami nilivyowaona nimewachukulia kama wengine wanavyokwenda kunywa chai”.

No comments: