Wednesday, November 17, 2010

TUCTA yaibuka, kuishitaki serikali tena

na Stephano Mango, Dodoma




NAIBU Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA), Nicholaus Mgaya, amesema wanatarajia kuifikisha mahakamani serikali kwa kosa la kuchakachua mishahara ya wafanyakazi wa sekta binafsi tofauti na makubaliano ya mwanzo waliyoafikiana.

Mgaya aliyasema hayo mjini hapa jana wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa mikutano wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), mkoani Ruvuma ambapo alisema Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya, alitangaza mishahara iliyochakachuliwa na kupunguzwa tofauti na makubaliano yao.

Alisema wao, walitaka sekta ya umma walipwe kima cha chini sh 135,000, ingawa utafiti wao walioufanya mwaka 2006 walitaka kima cha chini kiwe sh 315,000.

Alisema tayari wamefika Mahakama ya Kazi na kutoa notisi ya siku 30 ili kutekelezwa makubaliano yao ambayo walipanga kwenye vikao vyao kati ya viongozi wa TUCTA na serikali kuwa lazima mambo matatu yatekelezwe, ambayo ni kuongeza mishahara, kupunguzwa kodi pamoja na madai ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii.

“Tutaishitaki serikali Mahakama ya Kazi na tayari tumeshatoa notisi ya siku 30 na kinachosubiriwa sasa ni serikali kutujibu notisi yetu,” alisema Mgaya.

Akijibu swali la waandishi wa habari kama ana ugomvi na serikali, Mgaya alikanusha madai hayo na kusisitiza kuwa wao wanapigania haki za msingi.

Alisisitiza kuwa watadai madai yao wakiwa ndani ya misingi ya sheria na kanuni na taratibu za nchi zinavyosema bila kuvunja sheria zilizowekwa na kwamba bado wataendelea na madai yao kama walivyopanga mpaka kieleweke.

Mgaya yuko mkoani Ruvuma kwa ziara ya siku moja, ambapo alisema lengo la ziara hiyo ni kutembelea Kamati ya Mkoa ya shirikisho na kuingiza wanachama wapya.

No comments: