Sunday, July 24, 2011

IGP Mwema apangua makamanda

Na Daniel Mjema

INSPEKTA Jenerali wa Polisi (IGP), Said Mwema, amefanya mabadiliko ya safu ya uongozi wa makamanda wa polisi kwa baadhi ya mikoa ya Tanzania bara.

Katika mabadiliko hayo, baadhi ya makamanda wa mikoa wamehamishwa huku maofia 122 wakipandishwa vyeo.

Mabadiliko hayo yameambatana na uteuzi wa vyeo vya juu ambapo Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Tanzania, Rais Jakaya Kikwete, amewapandisha vyeo maofisa watano na kuwa Manaibu Kamishina.

Miongoni mwa waliopandishwa vyeo kutoka kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi(SACP) kuwa Manaibu Kamishina ni pamoja na Kamanda Simon Sirro.

Habari za uhakika ambazo Mwananchi Jumapili inazo zimesema katika mabadiliko hayo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Sirro amehamishiwa makao makuu ya Polisi Jijini Dar kuwa mkuu wa operesheni maalumu za Jeshi hilo.

Nafasi ya Kamanda Sirro imechukuliwa na aliyekuwa kamanda wa Polisi mkoa Tabora, Leberatus Lyimo, huku Ofisa Mnadhimu wa Polisi namba moja wa mkoa huo, Anthony Rutashugurugukwa, akiteuliwa kuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo.

Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Tabora(OCD), Yusuph Mruma, ameteuliwa kuwa Ofisa Mnadhimu namba moja wa Mkoa wa Tabora kuchukua nafasi ya Rutashugurugukwa.

Taarifakuhusu mabadiliko hayo iliyotolewa na IGP Mwema Julai 22 mwaka huu ambayo Mwananchi Jumapili imefanikiwa kuiona, inaeleza pia kuwa tume ya utumishi wa polisi na Magereza imewapandisha vyeo maofisa 117.

Kulingana na taarifa hiyo, maofisa 21 waliokuwa na vyeo vya warakibu wasaidizi waandamizi wa jeshi hilo (SSP), wamepandishwa vyeo na kuwa makamishina wasaidizi wa polisi(ACP) na kuwahamisha vituo vyao vya kazi.

Halikadhalika maofisa 96 waliokuwa na vyeo vya Mrakibu wa Polisi (SP) wamepandishwa vyeo na kuwa warakibu waandamizi wa polisi (SSP).

Baadhi ya waliohamishwa ni OCD Monduli, Contantine Maganga na Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Moshi, Zakaria Benard, wanaohamishiwa ofisi ya Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro ambapo watapangiwa majukumu mapya.

Wengine ni Kihenya Kihenya, ambaye ni OCD Kasulu aliyehamishiwa Mkoa wa Kigoma kuwa Ofisa Mnadhimu namba moja na Alicheus Mtalemwa, ambaye ni Ofisa Mnadhimu namba moja wa Kigoma anakuwa Ofisa Polisi Jamii mkoa Rukwa.

Katika taarifa hiyo ya kipolisi, IGP Mwema amewapongeza maofisa wote waliopandishwa vyeo na Tume ya polisi na Magereza na kwamba upandishwaji huo wa vyeo ulianza rasmi Juni 30 mwaka huu.

Msemaji wa jsehi hilo, Advera Sinso alithibitisha taarifa hizo, lakiniakasema: "Mi mabadiliko ya kawaida tu ya ndani."

Hakuweza kuweka wazi juu ya mabadiliko hayo kwa kile alichodai yuko Dodoma, nje ya makao makuu ya polisi ambayo yapo Dar es Salaa, hivyo akashauri afuatwe kesho.

No comments: