Monday, March 31, 2008

Fumanizi






Tukio hilo lilichukua nafasi Jumatano iliyopita (Machi 26), saa 6:15 mchana kwenye nyumba ya kulala wageni yenye jina la Timova Bar & Guest House, iliyopo Mbezi Mwisho, jijini.

Jopo la waandishi wetu, lilikuwepo kamili kushuhudia ‘muvi’ hiyo na lilifika mapema eneo la tukio, kwakuwa lilijulishwa siku mbili kabla, kuhusu kuwepo kwa mkakati huo wa kumshika mtu ugoni.

Jumatatu iliyopita, mume aliyefumania (jina tunalo), alipiga simu kwenye dawati la gazeti hili, akitaka waandishi wetu kufika Timova Gesti, Machi 26, 2008, saa sita mchana, wakiwa na kamera zao kwa ajili ya kupiga picha za tukio la fumanizi.
Alisema: “Kuna jirani yangu ambaye namheshimu sana, kwa jinsi tulivyo na ukaribu, mimi huwa namchukulia kama kaka yangu, lakini ananifanyia unyama kwa mke wangu, nimemvumilia nimeshindwa, nimeandaa mtego, nataka nimshikishe adabu.”

Baada ya kupata simu hiyo, gazeti hili lilitumia muda wake na kukutana ana kwa ana na mlalamikaji huyo Jumanne iliyopita, ili kupata ‘data’ za kutosha, kuhusu sekeseke hilo.

Katika maelezo yake, mume huyo alimtuhumu Ali a.k.a Ngosha kuwa, kwa muda mrefu amekuwa akimtaka kimapenzi mke wake (jina tunalificha) na kumhadaa kwamba atamfanyia mambo makubwa endapo angemkubalia.

“Mwanzoni mke wangu alikuwa haniambii, alinificha kwa kuogopa kuvunja ujirani wetu, lakini siku chache kabla ya Pasaka ya mwaka huu, Ngosha alivizia mimi sipo nyumbani, akamfuata mke wangu na kutaka kumbaka, tena chumbani kwangu.

“Ilibidi mke wangu afanye ujanja ili ajiokoe, kwa hiyo akafanya kama anamkubalia na kumuomba wapange siku nyingine, wakutane mbali na maeneo ya nyumbani kwetu, jamaa akawa amemkubalia,” alisema mume huyo.

Mtoa habari huyo alifafanua kwamba baada ya Ali Ngosha kukubali wazo hilo, aliiteua Timova kama sehemu muafaka ya kula ‘nanasi kwa nafasi’, pia akaipendekeza Machi 26, 2008 kuwa ndiyo siku ya kukata utepe wa penzi kati yao, mambo ambayo mwanamke huyo aliigiza kuyakubali.

Aliongeza: “Niliporudi, mke wangu alinipa ‘full story’, jinsi alivyoanza kumtongoza miezi miwili iliyopita, alivyotaka kumbaka, mpaka walivyokubaliana wakutane gesti. Nilishtuka sana! Mwanzoni sikuamini, lakini nilipofanya upelelezi wangu, niliamini.”

Habari zaidi ni kwamba siku ya tukio, Ijumaa Wikienda lilitinga kwenye gesti hiyo saa mbili asubuhi, kabla ya kumshuhudia Ngosha akiingia hapo takriban dakika 60 baadaye na kukodi chumba namba tatu.

Saa 6:08 mchana, mwanamke aliyekuwa akimezewa mate na ‘mgoni’ huyo, aliwasili katika gesti hiyo na kuwauliza wahudumu sehemu kilipo chumba namba tatu, kisha baada ya kuoneshwa aliingia ndani.

Dakika saba baadaye, mume mtu alifika akiwa ameongozana na timu ya watu sita na kuvamia chumba hicho, ambapo walimkuta Ngosha akiwa ameshachojoa nguo zote, wakati mwanamke alikuwa amejifunga taulo.


Aidha, habari zinaongeza kuwa baada ya mume mtu na timu yake kuingia chumbani, walianza kumshushia mkong’oto mgoni huyo, kabla ya kumfanyia kitu mbaya kwa kumvalisha shanga mwili mzima.
Hata hivyo, polisi walifika eneo la tukio na kumuokoa Ngosha mikononi mwa timu hiyo yenye hasira.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa Ngosha naye ana mke na watoto wawili (majina tunayahifadhi), pia uligundua kuwa majirani hao baada ya kufika polisi waliamua kusameheana, huku wakipeana onyo kwamba kila mtu asitamani cha mwenzake.

No comments: